Watu 14 wauawa katika mashambulio ya waasi mashariki mwa Kongo DR
Watu 14 wameuawa katika mashambulio yaliyofanywa na makundi yanayobeba silaha mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.
Hayo ni kwa mujibu wa duru za jeshi na maafisa wa mkoa wa Kivu Kaskazini yalikofanywa mashambulio hayo.
Msemaji wa jeshi katika eneo hilo Kapteni Guillaume Djike amesema mashambulio kadhaa yalifanywa jana usiku dhidi ya maeneo ya raia na ngome za vikosi vya serikali. Djike, amelituhumu kundi la waasi wa Mai-Mai kuwa ndilo lililohusika na mashambulio hayo.
Msemaji huyo wa jeshi ameeleza kuwa askari mmoja na raia mmoja waliuawa katika eneo la Kaunga, raia wanne waliuliwa kwa kupigwa risasi na kwa silaha baridi katika eneo la Kashalira na raia wengine saba waliuliwa katika eneo la Kibirizi katika shambulio lililofanywa na watu waliobeba silaha.
Wakati huohuo Roger Bihango, mwakilishi wa Gavana wa jimbo la Kivu Kaskazini ametangaza kuwa waasi wa Mai Mai walimpiga risasi na kumuua raia mmoja katika eneo la Buleusa.
Guillaume Djike ameongeza pia kuwa nyumba 150 zilichomwa moto katika mashambulio hayo ya jana usiku.
Mamia ya raia wameuawa katika mwaka uliopita katika machafuko na mauaji ya halaiki yaliyofanywa na makundi yanayobeba silaha katika mkoa wa Kivu Kaskazini wa mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo unaopakana na nchi za Rwanda na Uganda.../