Waasi wa Niger Delta nchini Nigeria watoa wito wa kusitishwa mapigano
Waasi wa eneo la Niger Delta nchini Nigeria wametoa wito wa kusitishwa mapigano katika eneo hilo la kusini mwa nchi hiyo.
Katika barua ya wazi waliyomwandikia Rais Muhammadu Buhari, waasi hao wametaka kuhitimishwa mapigano ya silaha na kutekelezwa usitishaji vita katika eneo hilo lenye utajiri mkubwa wa mafuta.
Katika barua hiyo imeelezwa kuwa muelekeo chanya na nia njema ya serikali ya Abuja utawezesha kutekelezwa usitishaji vita endelevu katika eneo la Niger Delta.
Katika barua hiyo kwa Rais Buhari, waasi wa Niger Delta mbali na kutangaza utayari wao wa kufanya mazungumzo na serikali kuhusiana na madai na matakwa yao wameeleza kwamba kutumwa vikosi vya jeshi katika eneo hilo hakutokuwa na tija yoyote.
Barua hiyo ya wanamgambo wa eneo la Niger Delta imeandikwa baada ya Rais wa Nigeria kutoa onyo kwa makundi ya waasi yanayobeba silaha katika eneo hilo kwamba serikali itaamiliana nayo kama inavyoamiliana na kundi la kigaidi na kitakfiri la Boko Haram. Buhari alitoa onyo hilo pembeni ya kikao cha "Mkutano wa Kimataifa wa Ustawi wa Afrika".
Wakati huohuo Gavana wa jimbo la Bayelsa, Henry Dickson amesema kutumwa vikosi vya jeshi pekee katika eneo la Niger Delta hakutoshi kwa ajili ya kukabiliana na mashambulio ya makundi ya waasi yanayolenga vinu na mabomba ya mafuta bali inapasa zichukuliwe hatua nyengine za lazima na kwa tahadhari.
Hii ni katika hali ambayo makundi yanayobeba silaha yameshambulia na kuripua vinu vya gesi katika eneo la Wascravos katika jimbo la Delta kusini mwa Nigeria.../