Genge la wanawake wenye uhusiano na Daesh watiwa mbaroni Morocco
Duru rasmi nchini Moroco zimearifu habari ya kutiwa mbaroni wanawake kumi wenye mfungamano na kundi la kigaidi la Daesh ambao walikuwa na lengo la kutekeleza mashambulizi ya kigaidi katika miji kadhaa nchini humo.
Wizara ya Mambo ya Ndani ya Morocco imeeleza kuwa wanawake hao kumi walikuwa wakijaribu kutafuta mada za kemikali zinazotumika kutengenezea mikanda ya kujiripua. Wanawake hao magaidi walikusudia pia kutekeleza mashambulizi ya kulipua mabomu katika taasisi muhimu za Morocco. Wizara ya Mambo ya Ndani ya Morocco imeeleza kuwa wanawake hao waliotiwa nguvuni walikuwa wana uhusiano wa karibu na magaidi kadhaa wa nchi hiyo wenye mfungamano na Daesh walio na makao yao katika mpaka wa Syria na Iraq. Wanachama wa kundi hilo la kigaidi wamekuwa wakitekeleza hujuma katika miji kadhaa ya Morocco.