Ethiopia yapitisha sheria kali zaidi za hali ya hatari
Wizara ya Ulinzi ya Ethiopia imetangaza habari ya kuanzisha sheria kali zaidi za hali ya hatari nchini humo.
Katika taarifa iliyopchapishwa leo Jumatatu na magazeti ya nchi hiyo, serikali ya Ethiopia imetangza kuwa, mabadilishano yoyote ya habari na maelezo hasa kupitia mitandao ya kijamii kuhusu kuandaa maandamano ya kisiasa ni kinyume cha sheria. Tayari mawasiliano ya simu za mkononi na Intaneti imekuwa vigumu kupatikana katika maeneo mengi ya Ethiopia kwa siku kadhaa sasa.
Aidha serikali ya Ethiopia imepiga marufuku utazamaji televisheni za satalaiti na radio zinazosimamiwa na kundi la wapinzani wa Oromo anaoishi nchi za kigeni.
Siku chache zilizopita, Hairemariam Desalegn Waziri Mkuu wa Ethiopia alitangaza hali ya hatari kwa muda wa miezi sita nchini humo ili kurejesha amani baada ya machafuko ya wiki kadhaa yaliyosababisha raia kadhaa kuuawa na vile vile kuathiri viwanda na mashamba ya maua yanayomilikiwa na raia wengi wa kigeni.
Kabla ya hapo, wafanya maandamano waliharibu makumi ya magari, na hivyo kuzidisha madhara ya kiuchumi kufuatia wimbi la ghasia na machafuko yaliyoikumba nchi hiyo kutokana na wananchi kulalamikia kuporwa ardhi na haki zao.
Serikali ya Ethiopia inasema machafuko na ghasia zilizotokea wiki iliyopita katika eneo la Oroma yamechochewa na maadui wa kigeni hususan Misri na Eritrea.