Kwa mara nyingine uchaguzi wa rais Somalia waahirishwa, tarehe haijulikani
Uchaguzi wa rais nchini Somalia uliokuwa umepangwa kufanyika tarehe 30 ya mwezi huu, umeahirishwa kwa mara ya tatu.
Vyombo vya habari nchini humo vimeripoti hii leo kwamba, uchaguzi huo utafanyika katika tarehe nyingine itakayotangazwa hapo baadaye. Tume ya uchaguzi ya Somalia imenukuliwa ikisema kuwa, hadi sasa haijafahamika uchaguzi huo utafanyika lini, ingawa imesema kuwa utafanyika kabla ya kumalizika mwaka huu.
Mwezi Agosti mwaka huu Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa lilionyesha masikitiko yake makubwa juu ya mwenendo wa ucheleweshaji wa uchaguzi huo na kuitaka serikali ya Mogadishu kuainisha tarehe mpya kwa ajili ya zoezi hilo muhimu. Kabla ya hapo pia Michael Keating mwakilishi maalumu wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa nchini Somalia alisema kuwa, uahirishwaji uchaguzi huo, utaiongezea jamii ya kimataifa wasi wasi juu ya usalama wake.
Somalia ambayo inafanya juhudi za kukarabati uharibifu wa miongo kadhaa iliyopita, inakabiliwa na mashambulizi ya wanachama wa kundi hatari la kigaidi na kitakfiri la ash-Shabab.