Uingereza yatuma mamia ya askari wake nchini Sudan Kusini
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i28588-uingereza_yatuma_mamia_ya_askari_wake_nchini_sudan_kusini
Serikali ya Uingereza imeanza kutuma askari 400 wa nchi hiyo nchini Sudan Kusini kwenda kujiunga na Kikosi cha Kulinda Amani cha Umoja wa Mataifa UNMISS.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
May 03, 2017 03:14 UTC
  • Uingereza yatuma mamia ya askari wake nchini Sudan Kusini

Serikali ya Uingereza imeanza kutuma askari 400 wa nchi hiyo nchini Sudan Kusini kwenda kujiunga na Kikosi cha Kulinda Amani cha Umoja wa Mataifa UNMISS.

Habari zinasema kuwa, kundi la kwanza la jeshi la Uingereza liliwasili mjini Juba jana Jumanne, kwenda kujiunga na wanajeshi 13,000 wa Umoja wa Mataifa ambao wamekuwa nchini humo tangu mwaka 2011, huku wanajeshi wengine wa nchi hiyo ya Ulaya wakitazamiwa kutumwa katika siku zijazo.

Inaarifiwa kuwa, kikosi hicho cha Uingereza kinajumuisha madaktari na wahandisi. Wahandisi wanatazamiwa kuelekea katika kambi za wakimbizi katika maeneo ya Bentiu and Malakal kaskazini mwa nchi kwa ajili ya kufanyia ukarabati miundombinu huku timu ya madaktari ikitumwa katika eneo la Bentiu ili kutoa huduma za matibabu kwa raia na askari 1,800 wa kikosi cha UN kilichoko katika eneo hilo.

Wanajeshi wa UN nchini Sudan Kusini

Haya yanajiri wiki 3 baada ya vikosi vya ardhini vya Japan kuanza kuondoka huko Sudan Kusini, baada ya kuwa katika nchi hiyo ya Kiafrika tangu mwaka 2012 kwa kile kilichotajwa kuwa kusaidia kujenga barabara na miundombinu mingine nchini humo. 

Sudan Kusini ilitumbukia katika mapigano ya ndani mwaka 2013, baada ya Rais Salva Kiir, kumtuhumu aliyekuwa makamu wake wa rais Riek Machar kwamba alipanga njama ya kutaka kumpindua madarakani. Hadi sasa maelfu ya watu wamekwishauawa na mamilioni ya wengine kuwa wakimbizi kutokana na machafuko hayo.