Waaasi wwili wauawa katika mapigano kaskazini mashariki mwa DRC
Waasi wawili wameuawa katika mapigano yaliyozuka baina yao na wanajeshi wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo katika jimbo la Ituri la kaskazini mashariki mwa nchi hiyo.
Carlos Kalombo, msemaji wa jeshi la Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo katika jimbo la Ituri amenukuliwa na vyombo vya habari vya nchi hiyo akisema kuwa, waasi wawili wa kundi linalojiita la wazalendo wa Ituri wameuawa kwenye mapigano na jeshi la nchi hiyo.
Aidha amesema jeshi la Kongo limefanikiwa kuwarudisha nyuma waasi hao katika maeneo ya pambizoni mwa kambi ya kijeshi iliyoko karibu na kijiji cha Kelenzi, mkoani Ituri.
Ameongeza kuwa, waasi hao wameripua bomu karibu ma shule ya kijiji cha Kelenzi na baadaye kudai kuwa wanajeshi wa serikali ndio walioripua bomu hilo. Aidha amekanusha madai kuwa wanajeshi wa serikali wanapora mali za raia.
Uhusiano baina ya makabila mbalimbali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo uko hatarini kutokana na mapigano ya muda mrefu na kuparaganyika familia pamoja na kuhama baadhi ya makabila na kuhamia maeneo ya makabila mengine.