Wakenya wakusanya akiba ya chakula kabla ya uchaguzi mkuu kesho Jumanne
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i32832-wakenya_wakusanya_akiba_ya_chakula_kabla_ya_uchaguzi_mkuu_kesho_jumanne
Wananchi wa Kenya ambao wamejawa na wasiwasi leo wamekuwa wakikusanya na kujiwekea akiba ya chakula huku polisi wakiwa tayari wameandaa masanduku ya huduma ya kwanza siku moja kabla ya uchaguzi mku wa kesho ambao wengi wanahofu kwamba huwenda ukaitumbukiza tena nchi hiyo katika hali ya mchafukoge.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
Aug 07, 2017 12:11 UTC
  • Wakenya wakusanya akiba ya chakula kabla ya uchaguzi mkuu kesho Jumanne

Wananchi wa Kenya ambao wamejawa na wasiwasi leo wamekuwa wakikusanya na kujiwekea akiba ya chakula huku polisi wakiwa tayari wameandaa masanduku ya huduma ya kwanza siku moja kabla ya uchaguzi mku wa kesho ambao wengi wanahofu kwamba huwenda ukaitumbukiza tena nchi hiyo katika hali ya mchafukoge.

Aidha baadhi ya familia zimeshuhidiwa zikisafiri kuelekea maeneo ya mashambani ya nchi hiyo kwa kuhofia machafuko. 

Kiongozi wa upinzani nchini Kenya, Raila Odinga mwenye umri wa miaka 72 ambaye alishindwa katika chaguzi za Rais za mwaka 2007 na 2013 amesema kuwa, Rais Uhuru Kenyatta mwenye umri wa miaka 55 hawezi kushinda uchaguzi wa kesho isipokuwa kama chama tawala cha Jubilee kitaiba kura, msimamo ambao unazidisha uwezekano wa kuibuka machafuko huko Kenya.

Uchunguzi wa maoni uliofanywa kabla ya uchaguzi wa Rais wa kesho unaonyesha kuwa wagombea hao wawili wa kiti cha urais wanakabana koo kwa koo yaani asilimia 50 kwa 50.  Katika uchaguzi wa kesho, wananchi wa Kenya watawachagua pia wabunge na wawakilishi wao wa kaunti.

Wakenya wenye wasiwasi katika kituo cha mabasi cha Nairobi wakisubiri kuelekea mikoani

Mwaka 2007, Raila Odinnga alitoa wito wa kufanyika maandamano kupinga matokeo ya uchaguzi baada ya kubainika kasoro katika zoezi la kuhesabu kura, hatua iliyochochea ghasia za kikabila ambapo watu wasiopungua 1200 waliuawa na wengine laki sita kulazimika kuyahama makazi yao.

Maduka ya bidhaa mbalimbali nchini Kenya yameshuhudiwa yakiwa yamejaa watu wengi wanaonunuza bidhaa za mahitajio kabla ya uchaguzi wa kesho.