Serikali ya DRC yawaita wapinzani katika meza ya mazungumzo
Serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo imewaita wapinzani wa nchi hiyo katika meza ya mazungumzo ili kujaribu kutatua hitilafu zilizoko kati ya pande mbili hizo.
Wito huo wa mazungumzo umetolewa na Joseph Kapika Waziri wa Uchumi wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo ambaye amewataka waandaaji wa maaandamano yaliyopigwa marufuku na Meya wa jiji la Kinshasa kuitikia wito wa serikali wa kuweko mazungumzo baina ya pande mbili.
Waziri huyo wa serikali ya Rais Joseph Kabila amesisitiza kuwa, serikali ya Kinshasa iko tayari kufanya mazungumzo na vyama vyote vya nchi hiyo na kwamba, matatizo na hitilafu zote zilizopo zinaweza kupatiwa ufumbuzi katika mazungumzo.
Kadhalika Waziri wa Uchumi wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo ameashiria maandamano ya utumiaji mabavu ambayo hutokea mara kwa mara nchini humo na kubainisha kwamba, malengo ya baadhi ya waandamanaji ni kuzusha machafuko na vitendo vya utumiaji mabavu.
Aidha Waziri Joseph Kapika amewataka wapinzani waachane na mpango wao wa maandamano waliyoyaitisha leo Jumatatu Septemba 4 akisisitiza kwamba, njia bora ya kutatua hitilafu ni kupitia mazungumzo.
Mgogoro wa ndani nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo uliibuka baada ya kuahirishwa tarehe ya uchaguzi wa rais na kadhalika sisitizo la Rais Joseph Kabila la kutaka kuendelea kusalia madarakani nchini humo. Licha ya kutiwa saini makubaliano baina ya wapinzani na serikali juu ya kufanyika uchaguzi wa rais tarehe 31 mwezi Disemba mwaka huu, hata hivyo inaonekana kuwa, uchaguzi huo hautaweza kufanyika katika tarehe iliyopangwa.