IMF: Uchumi wa Tanzania utadhoofika kutokana na sera za serikali
Mfuko wa Fedha wa Kimataifa (IMF) umetahadharisha kuwa, uchumi wa Tanzania utadhoofika iwapo sera za sasa na sheria mpya zitaendelea kutekelezwa.
Katika taarifa ambayo imechapishwa na Shirika la Habari la Reuters Alhamisi, ripoti iliyovuja ya IMF inaonyesha kuwa uchumi wa Tanzania, ambao ni wa tatu kwa ukubwa Afrika Mashariki, unakabiliwa na hatari ya kudorora.
Ripoti hiyo inasema ingawa Rais John Magufuli wa Tanzania anatekeleza mpango wa kuimarisha viwanda nchini humo lakini uwekezaji wa kigeni umepungua nchini humo kutokana na sera za serikali kuingilia sekta za uchimbaji madini na kilimo.
Benki ya Dunia inasema uwekezji wa moja kwa moja wa kigeni ulipungua hadi asilimia 2 katika Pato Ghafi la Taifa (GDP) mwaka 2017 kutoka asilimia 5 mwaka 2014.
Katika ripoti hiyo ambayo haikuzinduliwa rasmi ndani ya Tanzania baada ya wakuu wa serikali kutoidhinisha uchapishaji wake, IMF imesema mazingira dhaifu ya biashara na utekelezwaji wa miradi ambayo haiingizi pato kubwa la kifedha ni nukta zinazoweza kubana ustawi wa kila mwaka wa GDP na kuufanya kuwa chini ya asilimia 6.3 ambao ulikuwa ustawi kwa wastani kati ya mwaka 1998 hadi 2017.

IMF imetabiri kuwa ustawi wa GPD nchini Tanzania utakuwa baina ya asilimia 4-5 katika kipindi cha miezi sita iwapo sera za sasa zitaendelea. Utabiri huo wa IMF unatafautiana na makadirio ya serikali ya Tanzania kuwa uchumi wa Tanzania utastawi kwa asilimia 7.3 mwaka 2019.
Msemaji wa IMF amekataa kutoa maoni kuhusu taarifa hiyo ambayo imechapishwa na Reuters huku akisisitiza kuwa mfuko huo hautoi maoni kuhusu ripoti zilizovuja.