Watu zaidi ya 60 wapoteza maisha katika ajali ya boti DRC
(last modified Tue, 16 Feb 2021 07:55:58 GMT )
Feb 16, 2021 07:55 UTC
  • Watu zaidi ya 60 wapoteza maisha katika ajali ya boti DRC

Watu wasiopungua 60 wamefariki dunia kufuatia ajali ya boti magharibi mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.

Steve Mbikayi, Waziri wa Masuala ya Kibinadamu wa nchi hiyo amesema boti hiyo iliyokuwa imebeba abiria kupita kiasi ilighariki katika Mto Congo karibu na kijiji cha Longola Ekoti, mkoani Mai-Ndombe magharibi mwa nchi, usiku wa kuamkia jana.

Amesema kufikia sasa miili 60 imeopolewa kutoka kwenye maji ya mto huo, na kwamba walionusuriwa kufikia sasa ni watu 300. Waokoaji wanaendelea na kazi ya kutafuta miili na watu waliotoweka katika eneo hilo la magharibi mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.

Mbikayi amesema boti hiyo iliyokuwa imebeba watu zaidi ya 700 ilikuwa ikitokea Kinshasa, mji mkuu wa DRC ikielekea mkoa wa Equator kabla ya kutokea ajali hiyo.

Boti zinavyojaza abiria na mizigo kupita kiasi nchini DRC

Ajali za aina hii hutokea mara kwa mara kwenye mito na maziwa nchini humo, na sababu kuu ya ajali hizo ni hali mbaya za boti, kujazwa abiria kupita kiasi na kuzeeka kwa boti hizo.

Julai mwaka 2010, watu 135 walikufa maji baada ya boti yao kuzama katika mkoa wa Bandundu nchini DRC, moja ya ajali mbaya zaidi za majini kuwahi kuripotiwa nchini humo.