HRW: Watu 400 wameuawa katika maandamano dhidi ya serikali Ethiopia
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i9322-hrw_watu_400_wameuawa_katika_maandamano_dhidi_ya_serikali_ethiopia
Shirika la kutetea haki za binadamu la Human Rights Watch limesema mamia ya watu wameuawa katika maandamano ya wananchi dhidi ya serikali ya Ethiopia, kuanzia Novemba mwaka jana hadi sasa.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
Jun 16, 2016 11:01 UTC
  • HRW: Watu 400 wameuawa katika maandamano dhidi ya serikali Ethiopia

Shirika la kutetea haki za binadamu la Human Rights Watch limesema mamia ya watu wameuawa katika maandamano ya wananchi dhidi ya serikali ya Ethiopia, kuanzia Novemba mwaka jana hadi sasa.

Ripoti iliyotolewa leo Alkhamisi na shirika hilo lenye makao makuu yake mjini New York nchini Marekani imesema kuwa, watu 400 wakiwemo watoto wadogo wameuawa baada ya maafisa usalama kutumia nguvu kupita kiasi kuzima maandamano ya wananchi ambao wamekuwa wakiandamana dhidi ya serikali ya Addis Ababa.

Hata hivyo Getachew Reda, msemaji wa serikali ya nchi hiyo ya Pembe ya Afrika amekanusha madai hayo na kusisitiza kuwa idadi hiyo 'imetiwa chumvi' na Human Rights Watch. Amesema kuwa serikali inasikitika kutokana na mauaji ya raia na maafisa usalama, kwa sababu ya machafuko yanayochochewa na makundi ya upinzani ya ndani na nje ya nchi.

Mwezi Februari mwaka huu, serikali ya Ethiopia ilikanusha madai yaliyotolewa na baadhi ya ripoti za mashirika ya kutetea haki za binadamu kwamba, imefanya ukandamizaji dhidi ya raia wake katika eneo la Oromia. Mashirika hayo yalisema kuwa, vikosi vya serikali ya Ethiopia vimetumia nguvu kupita kiasi kuzima maandamano hayo yaliyoanza Novemba mwaka jana kupinga mpango wa kupanua mamlaka ya jiji kuu la Addis Ababa.