Apr 19, 2024 11:23 UTC
  • Sheikh Akbari: Operesheni ya Ahadi ya Kweli ni Kimbunga cha al Aqsa cha Iran

Khatibu wa Sala ya Ijumaa iliyosaliwa leo hapa Tehran amesema kuwa, operesheni iliyofanywa na Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ya kulipiza kisasi jinai za Israel ilikuwa ni kimbunga cha al Aqsa cha Iran dhidi ya utawala wa Kizayuni na ni operesheni ya kujivunia na kujifakharisha nayo.

Shirika la habari la Mehr limenukuu Hujjatul Islam Walmuslimin, Haj Ali Akbari akisema hayo kwenye khutba za Sala ya Ijumaa ya leo hapa Tehran na kuongeza kuwa, msingi mkuu katika majukumu ya kijamii ni msingi wa usalama na utulivu kwenye jamii hiyo. 

Amesema, dini tukufu ya Kiislamu imetenga misingi minne ya kuhakikisha usalama na amani inapatikana katika jamii. Ametoa mfano kwa kutaja misingi mwili akisema kuwa, msingi wa kwanza ni dhamana ya kiimani na kiitikadi kiasi kwamba Mwenyezi Mungu ameitanguliza haki ya watu mbele ya haki Yake. Jambo la pili la kudhamini usalama na amani katika jamii ni dhamiri ya ndani ya nafsi ya kila mtu ambayo ni hazina kubwa inayomfanya kila mtu apende mambo mazuri na achukie mambo mabaya.

Amma kuhusu majibu makali yaliyotolewa na Iran dhidi ya utawala wa Kizayuni, Khatibu wa muda wa Sala ya Ijumaa ya Tehran amesema kuwa, operesheni hiyo imeonesha nguvu kubwa za Jamhuri ya Kiislamu na udhaifu wa kuchupa mipaka wa utawala wa Kizayuni ambao licha ya kuwa na taarifa mapema ya kufanyika shambulio la Iran, lakini Israel na washirika wake walishindwa kuzuia shambulizi hilo. 

Amesema kwa kweli operesheni ya Ahadi ya Kweli ilikuwa ni operesheni na jihadi ya taifa zima la Iran lakini kwa msaada wa Mwenyezi Mungu na kusisitiza kuwa, jeshi la Iran ndilo jeshi la wananchi zaidi duniani.