Jul 01, 2024 03:00 UTC
  • Jenerali Safavi: Israel 'inayoporomoka' imeshindwa vibaya na muqawama

Mshauri Mkuu wa Ayatullah Sayyid Ali Khamenei, Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu katika masuala kijeshi amesema mrengo wa muqawama umefanikiwa kuushinda na kuusababishia vipigo utawala wa Kizayuni ambao upo katika ncha ya kuporomoka na kusambaratika.

Meja Jenerali Yahya Rahim Safavi alisema hayo jana Jumapili na kuongeza kuwa, "Katika tathmini ya kistratejia, wao (utawala wa Kizayuni) wameshindwa na mrengo wa muqawama, kuanzia Hizbullah ya Lebanon, Ansarullah ya Yemen, muqawama wa Syria na Iraq, hadi makundi ya muqawama ya Palestina."

Amesisitiza kuwa, waziri mkuu wa utawala wa Kizayuni, Benjamin Netanyahu ameshindwa na kudhalilishwa na makundi ya muqawama katika eneo hili hasasi na la kistratejia, na hajaweza kufikia hata lengo moja la kuushambulia Ukanda wa Gaza.

Ameeleza bayana kuwa, stratejia ya muqawama katika eneo hili la Asia Magharibi inazidi kuimarika na kupata nguvu, na hakuna shaka nguvu hizo zitafelisha njama za kambi ya ubeberu.

Makundi ya muqawama katika eneo

Meja Safavi amebainisha kuwa, stratejia ya muqawama ni kubadilisha mlingano wa nguvu katika mfumo wa kimataifa, na Mapinduzi ya Kiislamu yaliweka msingi wa kuundwa na kupanuliwa muqawama kote duniani. 

Ameongeza kuwa, muqawama unazidi kuimarika na kupata nguvu, na hakuna shaka utasambaratisha ubabe wa mataifa ya kibeberu na utawala haramu wa Israel unaoendelea kuua watoto na wanawake wa Kipalestina katika Ukanda wa Gaza.

Mshauri huyo Mkuu wa Amirijeshi Mkuu wa vikosi vyote vya ulinzi vya Iran amesisitiza kuwa, "Kambi ya muqawama imebadilisha mlingano wa nguvu katika maeneo yote ya Wapalestina yanayokaliwa kwa mabavu, upande wa kaskazini na kusini.

Tags