Rouhani: Iran inataka kuboresha uhusiano na eneo zima
Rais wa Iran amesema kuwa nchi hii inataka kuboresha uhusiano katika eneo zima la Ghuba ya Uajemi na kwamba lengo la mwisho la Tehran ni kuona amani na uthabiti zaidi inakuwepo katika eneo hili na nchi zote zinastawi.
Rais Hassan Rouhani ameashiria leo asubuhi katika mkutano na waandishi habari kabla ya kuelekea katika ziara ya siku moja huko Oman na Kuwait hatua ya nchi wanachama wa Baraza la Ushirikiano la Ghuba ya Uajemi ya kuunga mkono kuimarisha uhusiano na Iran na kuongeza kuwa serikali ya Kuwait imeitumia Tehran ujumbe kutoka nchi sita za pambizoni mwa Ghuba ya Uajemi ambazo zimeonyesha irada ya kuwa na uhusiano bora na Iran, kuzipatia ufumbuzi suutafahumu zilizopo na kuimarisha uhusiano wao na Iran kupitia kufanya mazungumzo.
Rais Rouhani amesema siasa za Iran zimejengeka katika msingi wa nia njema na majirani zake na kushirikiana na nchi za Kiislamu na kwamba Iran kamwe haifikirii kuivamia, kuiingilia kati, kuitwisha itikadi zake kidini, kimadhehebu au kisiasa nchi yoyote ile. Rais wa Iran amebainisha kuwa usalama wa Ghuba ya Uajemi una umuhimu wa kipekee kwa Iran na kwamba usalama wa eneo hili unapasa kudhaminiwa na nchi za eneo hilihili. Amesema kuwepo nchi ajinabi katika Ghuba ya Uajemi kumekuwa ni kwa madhara siku zote. Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran leo asubuhi ameelekea Muscat Oman kufuatia mwaliko rasmi wa Mfalme wa nchi hiyo lengo likiwa ni kufanya mazungumzo ya pande mbili na mfalme wa nchi hiyo. Mchana huu wa leo Rais Rouhani ataondoka Muscat na kuelekea ziarani nchini Kuwait.