Boroujerdi: Afghanistan na Afrika walengwa wa baadaye wa Daesh
Mkuu wa Kamisheni ya Usalama wa Taifa na Siasa za Nje ya Majlisi ya Ushauri ya Kiislamu ya Iran (Bunge) ameeleza kuwa magaidi wa kundi la Daesh sasa wameelekea nchini Afghanistan na watajipenyeza pia katika nchi za Kafrika kama ilivyokuwa huko nyuma.
Alauddin Boroujerdi amesema kuhusiana na mustakbali wa kundi la kigaidi la Daesh kwamba kundi hilo limepata pigo huko Syria na Iraq likiwa kama taasisi ya kijeshi na kisiasa; na kwamba Washington ilikuwa imeainisha muda wa kwa uchache miaka 20 ili kuweza kusambaratishwa kundi la Daesh.
Mkuu wa Kamisheni ya usalama wa Taifa na Siasa za Nje ya Majlisi ya Ushauri ya Kiislamu ya Iran amebainisha kuwa fikra za Kidaesh zitaendelea katika mkondo wake kwa miaka kadhaa na kwamba fikra hizo zimetokana na mafundisho ya Kiwahabi na uvumbuzi wa mashirika ya kijasusi ya Marekani na Uingereza.
Boroujerdi ameongeza kuwa, vitendo vinavyotekelezwa na makundi ya kigaidi vitawagharimu waungaji mkono wa magaidi hao na kwamba kuwepo raia wa Ulaya katika kundi la Daesh kunadhihirisha ukweli huu kuwa nchi zilizousababishia matatizo ulimwengu wa Kiislamu hivi sasa zenyewe ndizo zinazotaabika na hujuma za kigaidi.