Qassemi: Madola huru yasimame kukabiliana na saiasa za kibeberu za Marekani
Msemaji wa Wizara ya Mashauri ya Kigeni ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema kuwa, kikao cha pande tatu cha Iran, Afghanistan na India kuhusiana na kuimarisha ushirikiano wa kieneo kilikuwa na mafanikio.
Bahram Qassemi amesema hayo leo katika mkutano wake wa kila wiki na waandishi wa habari wa ndani na wa nje ambapo akijibu swali la mwandishi wa habari wa Shirika la Habari la Matangazo ya Ng'ambo la Iran kuhusiana na kikao cha pande tatu cha Iran, Afghanistan na India mjini Kabul kilichohudhuriwa na Manaibu Mawaziri wa Mashauri ya Kigeni wa nchi tatu hizo amesema kuwa, kufanyika vikao kama hivyo kunaweza kuwa na taathira chanya katika kustawisha ushirikiano wa kieneo.
Msemaji wa Wizara ya Mashauri ya Kigeni ya Iran amesema kuwa, madola huru yanapaswa kusimama na kukabiliana na siasa za kibeberu na kiistikbari za Marekani.
Bahram Qassemi ameashiria tukio la kuchomwa moto ubalozi mdogo wa Iran mjini Basra, Iraq na kushambuliwa ubalozi wa Iran mjini Paris, Ufaransa na kusema kuwa, matukio hayo mawili hayana uhusiano.
Msemaji wa Wizara ya Mashauri ya Kigeni ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema kuhusiana na matamshi ya Mike Pompeo, Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Marekani yaliyo dhidi ya Iran kuhusiana na uhusiano wa Tehran na serikali ya China na mazingira ya Waislamu wa nchi hiyo na kusema, watawala wa Marekani si wakweli bali kila wanachofikiria wao ni kulifanyia uadui tu taifa la Iran.