Rouhani: Taifa la Iran limeibuka na unshindi katika vita ya kiuchumi
-
Rais Hassan Rouhani
Rais Hassan Rouhani wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema kuwa taifa la Iran limeibuka na ushindi katika vita ya kiuchumi.
Akihutubia kikao cha Kamati ya Uratibu wa Masuala ya Uchumi mapema leo mjini Tehran, Rais Rouhani amesema kuwa, takwimu za ustawi wa uzalishaji katika sekta mbalimbali za viwanda hapa nchini ni ushahidi bora zaidi wa kufeli siasa za mashinikizo ya kiwango cha juu za Marekani ambazo Wamarekani wenyewe wamekiri kuwa zimeshindwa.
Rais Rouhani amesema kuwa, kwa kutilia maanani mazungumzo ya hivi karibuni huko Vienna, Wamarekani wametangaza waziwazi kwamba wako tayari kufuta vikwazo vyao dhidi ya Jamhuri ya Kiislamu. Amesema Iran itaendelea kushiriki katika mazungumzo hayo.
Amesema kuwa sekta ya viwanda vya kutengeneza magari ya Iran ambayo iliweza kushamili na kusimama ngangari katika kipindi kigumu na kuzidisha uzalishaji wake, itapiga hatua zaidi baada ya kufunguliwa milango ya kuingia katika masoko ya kimataifa.
Gazeti la New York Times la Marekani limeandika kuwa, uhakika mchungu ni kwamba mashinikizo ya kiwango cha juu dhidi ya Iran yamefeli na kushindwa.
Baraza la Wahariri wa wa gazeti la New York Times mwezi uliopita wa Aprili lilisema kuwa, uhakika mchungu ni kwamba, mashinikizo ya kiwango cha juu hayakuweza kubadili mienendo ya Iran bali kinyume chake, Tehran iliiadhibu Marekani kwa kusitisha utekelezaji wa baadhi ya vipengee vya makubaliano hayo ya nyuklia kwa sababu ya Washington kujiondoa katika makubaliano hayo, na kuifundisha Marekani jinsi dunia inavyokuwa bila ya makubaliano ya JCPOA.