Apr 28, 2024 11:45 UTC
  • Uwezekano wa ICC kutoa waranti wa kukamatwa Netanyahu kwa mauaji ya Ghaza umeitia tafrani Israel

Baraza la mawaziri la utawala haramu wa Kizayuni wa Israel limeingiwa na tafrani na wasi wasi mkubwa juu ya uwezekano wa Mahakama ya Kimataifa ya Jinai (ICC) kutoa waranti wa kukamatwa waziri mkuu wa utawala huo Benjamin Netanyahu na maafisa wengine waandamizi kwa kuhusika na jinai za vita vya miezi kadhaa vya mauaji ya kimbari dhidi ya Wapalestina wa Ukanda wa Ghaza uliozingirwa.

Vyombo vya habari vya Israel vimeripoti leo kuwa, maafisa wakuu wa Israel wamefanya mikutano ya dharura mjini Tel Aviv wiki hii kujadili uwezekano wa mahakama kuu ya Umoja wa Mataifa kutoa hati za kukamatwa Netanyahu, waziri wa vita Yoav Gallant, na mkuu wa majeshi Herzi Halevi.
 
Gazeti la lugha ya Kiebrania la Maariv limenukuu vyanzo ambavyo havikutajwa vikisema, Netanyahu alikuwa "na hofu na wasiwasi usio wa kawaida" kutokana na uwezekano wa kutolewa waranti wa kumtia nguvuni na mahakama ya  ICC yenye makao yake The Hague.
Netanyahu

Katika siku za hivi karibuni, Netanyahu amewapigia simu viongozi na maafisa wa kimataifa hususan Rais Joe Biden wa Marekani kumtaka azuie kutolewa waranti wa kumkamata.

Hayo yanajiri katika hali ambayo, katika kile kinachoonekana kama hatua ya kupinga dhahiri kutolewa kwa hati hiyo inayoripotiwa kuwa yamkini ikatolewa mnamo "siku chache zijazo," waziri mkuu huyo wa utawala wa Kizayuni alisema Ijumaa kwamba uamuzi wa ICC hautaathiri vita vyake huko Ghaza, ambavyo hadi sasa vimesababisha vifo vya Wapalestina zaidi ya 34,000. 

 
"Maamuzi yaliyopitishwa na mahakama huko Hague hayataathiri hatua za Israel," amedai Netanyahu.
 
Utawala wa Kizayuni wa Israel umepuuza hukumu ya awali iliyotolewa na Mahakama ya Kimataifa ya Haki ICJ mwezi Januari iliyoutaka uchukue hatua zote kulinda maisha ya raia huko Ghaza na kujiepusha na vitendo vya mauaji ya kimbari.../

 

Tags