Sheikh Nabil Qaouk: Saudi Arabia haina ubavu wa kukabiliana na Hizbullah
Naibu Mkuu wa Baraza la Utendaji la Harakati ya Hizbullah ya Lebanon kwa mara nyingine tena amekosoa vikali siasa za kuharibu mambo za utawala wa Saudi Arabia katika Mashariki ya Kati.
Sheikh Nabil Qaouk amesisitiza kuwa, siasa hizo za uharibifu za watawala wa Aal Saud ni doa baya kwa nchi za Kiarabu.
Naibu Mkuu wa Baraza la Utendaji la Harakati ya Hizbullah ya Lebanon ameashiria njama zisizo na natija za Saudia na utawala haramu wa Israel zinazolenga kutoa pigo kwa mhimili wa muqawama na kusisitiza kwamba, siasa za Riyadh zimeendelea kuwa mzigo mzito kwa mataifa ya Mashariki ya Kati.
Akihutubia kusini mwa Lebanon kwa mnasaba wa kumbukumbu ya mwaka wa 10 ya vita vya utawala wa Kizayuni wa Israel dhidi ya Harakati ya Hizbullah, Sheikh Nabil Qaouk amesisitiza kuwa, Israel na Saudia hazina ubavu wa kukabiliana na Hizbullah au kuidhoofisha harakati hiyo.
Naibu Mkuu wa Baraza la Utendaji la Harakati ya Hizbullah ya Lebanon amebainisha kuwa, umewadia sasa wakati wa kuadhimisha miaka kumi ya ushindi wa Hizbullah, kufichua sura iliyofichika ya utawala wa Saudi Arabia ambapo mwaka 2006, utawala huo ulikuwa mshirika wa Israel katika kuwauwa kwa umati wananchi wa Lebanon.
Ameongeza kuwa, baada ya kuondolewa kizoro, sasa sura halisi ya utawala wa Saudia inaonekana vyema.
Afisa huyo wa ngazi za juu wa Hizbullah ya Lebanon ameashiria mazungumzo ya Saudia na utawala haramu wa Israel na kusema kuwa, kwa hakika hatua ya Saudia ya kuwa na uhusiano na Israel imewadhalilisha mno Waarabu.
Hayo yanajiri katika hali ambayo, himaya na uungaji mkono wa Saudi Arabia ikishirikiana na utawala ghasibu wa Israel kwa makundi ya kigaidi katika Mashariki ya Kati imekabiliwa na radiamali mbalimbali za nchi, shakhsia na mirengo mbalimbali ya kisiasa katika eneo hili.