Israel inakalia kwa mabavu asilimia 85 ya ardhi za Palestina
Utawala wa Kizayuni wa Israel unakalia kwa mabavu asilimia 85 ya ardhi zote za Wapalestina.
Hayo ni kwa mujibu wa ripoti Idara Kuu ya Takwimu Palestina ambayo imetangazwa leo kwa mnasaba wa Siku ya Ardhi ambayo inaadhimishwa leo Palestina. Taarifa hiyo imesema kilomita mraba 27 elfu za ardhi za Palestina zimeghusibiwa na Wazayuni. Aidha taarifa hiyo imesema hivi sasa Wapalestina wanashikilia asilimia 15 tu ya ardhi zao ambapo asilimia 48 ya Wapalestina wanaishi katika ardhi hizo.
Taarifa hiyo imesema mwaka 1967, utawala wa Kizayuni ulichukua udhibiti wa asilimia 40 ya ardhi za Palestina katika Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan na baada ya hapo Wazayuni walipora ardhi zaidi za Wapalestina.
Idara Kuu ya Takwimu Palestina imesema utawala wa Kizayuni unaendeleza sera za kubomoa nyumba za Wapalestina na kutowapa idhini ya kujenga nyumba huku Wazayuni wakiruhusiwa kujenga vitongoji katika ardhi zilizoporwa za Wapalestina katika Quds Tukufu na maeneo mengine.
Ikumbukwe kuwa, Disemba 6 mwaka jana Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa lilipasisha azimio nambari 2334 ambalo lililaani ujenzi wa vitongoji vya walowezi wa Kizayuni unaofanywa na utawala wa Kizayuni wa Israel katika maeneo ya Wapalestina. Hata hivyo utawala wa Israel umekaidi matakwa ya dunia na kuendelea kujenga vitongoji hivyo.