HAMAS: Tunajiandaa kwa mapambano ya kuzikomboa ardhi zote za Palestina
Msemaji wa Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina (HAMAS) ametangaza kuwa, harakati hiyo inajiandaa kwa ajili ya mapambano ya kuzikomboa ardhi zote za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu na utawala haramu wa Israel.
Sami Abu Zuhri ameyasema hayo kutokana na hali ya mgogoro inaoendelea katika eneo la Quds na Msikiti wa al-Aqsa kufuatia ukandamizaji na ukatili unaofanywa na utawala wa Kizayuni wa Israel na kusisitiza kuwa, maeneo jirani na kibla hicho cha kwanza cha Waislamu yana jukumu ya kuulinda msikiti huo.
Sambamba na kusisitiza kwamba, hii leo muqawama umeshika kasi katika eneo la Quds, Abu Zuhri amesema kuwa, raia wa Palestina wamefungua ukurasa mpya wa mapambano kwa ajili ya kuhitimisha uvamizi wa utawala wa Kizayuni wa Israel. Msemaji wa HAMAS amelaani vikali njama za baadhi ya viongozi wa nchi za Kiarabu za kuboresha mahusiano yao na utawala huo khabithi wa Israel. Tangu Ijumaa iliyopita ya tarehe 14 Julai 2017, Israel ilishadidisha siasa za ukandamizaji dhidi ya Wapalestina katika Msikiti wa al-Aqsa.
Miongoni mwa ukandamizaji huo ni kuwazuia Wapalestina kuingia katika Msikiti wa al Aqsa, suala ambalo limeifanya hali ya mambo kuwa mbaya zaidi. Wakati huo huo, makundi ya Palestina yametangaza kuwa, Wapalestina hawatatekeleza marufuku iliyowekwa na Israel katika Msikiti wa al-Aqsa na kusisitiza kuwa, ikiwa utawala wa Kizayuni hautoondoa vizuizi ulivyoviweka katika msikiti huo, basi utapata jibu kali.