Syria: Tunaifahamu Marekani kama adui yetu na muungaji mkono wa magaidi
Faisal Mekdad, Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Syria amesema kuwa makundi ya kigaidi yanayochafua usalama wa nchi hiyo yanaungwa mkono kikamilifu na kusaidiwa na Marekani na kwamba Washington ni adui mkubwa wa Syria.
Al-Mekdad ameyasema hayo Jumapili ya jana katika mahojiano na kanali ya al-Mayadin ya nchini Lebanon na kusisitiza kuwa, Wamarekani kupitia njama zao za uungaji mkono kwa makundi ya kigaidi, wamesababisha uharibifu mkubwa kwa miundombinu ya taifa la Syria. Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Syria ameongeza kuwa, ni vyema Wamarekani kuhitimisha uwepo wao nchini Syria kwa ni kinyume na hivyo Damascus itaitangaza nchi hiyo kama adui aliyevamia ardhi ya Syria.
Kadhalika Faisal Mekdad, amezungumzia mapigano makali katika mji wa Deir ez-Zor na kusema kuwa, uungaji mkono wa Wamarekani kwa makundi ya kigaidi ndio uliyafanya magaidi hayo kuvamia hata mji huo. Jumanne iliyopita sambamba na jeshi la Syria na muqawama kuvamia kambi ya jeshi ya kikosi namba 137 magharibi mwa mji huo, ilivunja kikamilifu mzingiro wa zaidi ya miaka mitatu wa makundi ya kigaidi. Kufuatia hali hiyo, Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Syria akibainisha kuwa mji wa Deir ez-Zor ni moja ya maeneo ya kistratijia ambalo linazitenganisha Iraq na Syria, amesema kuwa Washington haitaki kuziona Damascus na Baghdad zikiwa na uhusiano mzuri.
Kadhalika ameshukuru uungaji mkono wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, Harakati ta Kiislamu ya Hizbullah na Russia kutokana na mchango wao katika vita dhidi ya ugaidi na kuongeza kuwa, Syria inazishukuru sana pande hizo.