Wabunge Pakistan walalamikia kunyongwa raia 66 wa nchi hiyo huko Saudia
Wawakilishi wa bunge la seneti nchini Pakistan wamelaani hatua ya kunyongwa raia 66 wa nchi hiyio katika kipindi cha miaka mitano pekee iliyopita huko nchini Saudi Arabia.
Wabunge wa Pakistan wameitaka Wizara ya Mambo ya Nje ya nchi hiyo kutoa maelezo ya kina kuhusiana na wimbi la kunyongwa kwa wingi raia wa Pakistan na mahakama za Saudi Arabia. Awali Wizara ya Mambo ya Nje ya Pakistan ilikuwa imetangaza kwamba, katika kipindi cha miaka mitano iliyopita, mahakama za Saudi Arabia zimewanyonga Wapakistan 66 kwa tuhuma tofauti.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, hadi sasa serikali ya Saudi Arabia imewatimua makumi ya maelfu ya raia wa Pakistan ikiwa pia inawashikilia maelfu ya wengine katika jela zake. Hii ni katika hali ambayo, licha ya Wapakistan kupinga nchi yao lao kushirikiana na Saudia katika muungano vamizi unaoongozwa na Riyadh dhidi ya Yemen, bado serikali ya Islamabad imeendelea kushirikiana na nchi hiyo kwa kutuma askari wake huko Saudia. Utawala wa kifalme wa Saudia umekuwa ukikosolewa mara kwa mara na mashirika mbalimbali ya haki za binaadamu kutokana na ukandamizaji mkubwa unaoufanya dhidi ya raia wa kigeni na wapinzani wa serikali.
Katika uwanja huo, Saudi Arabia imekuwa ikiwahukumu na kuwanyonga idadi kubwa ya watu kwa tuhuma hata nyepesi, suala ambalo limezitia wasi wasi mkubwa asasi za kiraia. Mbali na hayo ni kwamba Saudia inakosolewa kwa kutesa wafungwa na kuwashikilia katika mazingira mabaya mno watu wengi.