Trump aonya: Kutakuwa na 'umwagaji mkubwa wa damu' nisipochaguliwa kuwa rais wa Marekani
Donald Trump ameuambia mkutano wa hadhara katika jimbo la Ohio kwamba uchaguzi wa rais wa Novemba utakuwa "tarehe muhimu zaidi" katika historia ya Marekani akiitaja kampeni yake ya kuingia tena Ikulu ya White kama hatua ya mabadiliko muhimu sana kwa nchi hiyo.
Mapema mwezi huu Trump na Biden kila mmoja alishinda wajumbe wa kutosha kushinda uteuzi katika vyama vyao katika kinyang'anyiro cha urais wa 2024, ili kuchuana tena kwa kuzindua moja ya kampeni ndefu zaidi za uchaguzi katika historia ya Marekani.
Miongoni mwa masuala ambayo Trump anayafanyia kampeni ni mageuzi makubwa ya kile anachokiita sera za uhamiaji za "onyesho la kutisha" la Biden, licha ya kufanikiwa kuwashinikiza Warepublican kuzuia mswada wa Bunge la Congress ambao ulijumuisha hatua kali zaidi za usalama za mpakani kuwahin kuchukuliwa katika miongo kadhaa.
Siku ya Jumamosi alichochea tena suala la mpaka alipowafikia wapiga kura wa jamii za wachache ambao kijadi hupigia kura chama cha Democrat.
Alisema Biden "amewachoma kisu mgongoni wapiga kura Wamarekani wenye asili ya Afrika kwa kutoa vibali vya kufanya kazi kwa "mamilioni" ya wahamiaji, akionya kwamba Wamarekani weusi na Wamarekani wenye asili ya Kilatini "ndio watakaoteseka zaidi."
Kwa miongo kadhaa Ohio imekuwa ikionekana kama jimbo la mpambano, ingawa imekuwa ikionekana zaidi kuwa ngome ya Republican tangu Trump alipoingia White House katika uachaguzi wa 2016.
Mkutano wa jana umefanyika siku moja baada ya makamu wa rais wa zamani wa Trump, Mike Pence, kusema hatamuidhinisha bosi wake wa zamani kwa muhula wa pili katika Ikulu ya White House.../