Mar 22, 2024 02:30 UTC
  • UNICEF: Israel inaendesha

Msemaji wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto UNICEF James Elder amesema matukio yanayojiri katika Ukanda wa Ghaza ni "vita dhidi ya watoto," na kusisitiza kuwa eneo hilo hivi sasa si mahala pa kuishi watoto.

Akizungumza na shirika la habari la Anadolu, Elder amesema alitembelea Ghaza kwa mara ya pili tangu mashambulizi ya Oktoba 7 na kubainisha hali ya "kukata tamaa sana na kuchoka kwa kiwango cha kupindukia miongoni mwa watu."
 
Msemaji wa UNICEF ameelezea pia hali mbaya ya Hospitali ya Nasser huko Khan Younis, kusini mwa Ghaza, inayoshughulikia zaidi watoto waliojeruhiwa.
 
"Hospitali ya Nasser, ambayo ilikuwa hospitali muhimu sana, hasa kwa watoto waliojeruhiwa, haifanyi kazi tena," ameeleza afisa huyo wa UN.
 
James Elder ameendelea kubainisha kuwa UNICEF inavitambua vita vinavyoendeshwa na Israel katika Ukanda wa Ghaza kuwa ni 'vita dhidi ya watoto', kwa sababu, kwa kawaida, katika vita vyote, watoto ndio walio hatarini na wanaothirika zaidi, ambapo karibu asilimia 20 ya wanaofariki katika vita huwa ni watoto, lakini kwa upande wa Ghaza idadi hiyo ni karibu asilimia 40.
James Elder

Amefafanua kwa kusema: "zaidi ya watoto 10,000 wameuawa, na idadi inaendelea kuongezeka. Hatujui ni wangapi wako chini ya vifusi. Hili ni balaa kubwa kwa watoto. Watoto wengi wana njaa, na baa la njaa limeshakaribia."

Msemaji wa UNICEF ameeleza pia kuwa watoto huko Ghaza wanakabiliwa na matatizo mengi ya kisaikolojia na kuongeza kwamba njia pekee ya kutibu watoto hao ni kuanza na "usitishaji mapigano."

Ametoa indhari kwa kusema: Ghaza si mahali salama kwa watoto hivi sasa wakati kuna watoto zaidi ya milioni moja katika eneo hilo. Kwa hivyo, inabidi upatikane usitishaji vita kwanza, na kisha kuhakikisha watoto hao wanapata huduma zote wanazohitaji.

Wapalestina wanaokaribia 32,000, wengi wao wakiwa wanawake na watoto, wameuawa shahidi na zaidi ya 74,000 wamejeruhiwa katika Ukanda wa Ghaza  tangu jeshi la utawala haramu wa Israel lilipoanzisha vita vya mashambulio ya kinyama na mauaji ya kimbari katika eneo hilo Oktoba 7, 2023.../

Tags