Shambulizi la bomu dhidi ya hospitali Pakistan laua 50
Makumi ya watu wameuawa katika mlipuko wa bomu uliolenga hospitali kuu ya mji wa Quetta, kusini magharibi mwa Pakistan.
Habari zinasema kuwa, watu 52 wameuawa na makumi ya wengine kujeruhiwa baada ya bomu kuripuka katika chumba cha dharura cha hospitali hiyo ambacho kilikuwa na mawakili. Imearifiwa kuwa mawakili hao walikuwa katika hospitali hiyo kuchukua mwili wa mwenzao aliyeuawa kwa kupigwa risasi masaa machache kabla ya mripuko huo kutokea.
Sarfaraz Bugti, rais wa zamani wa chama cha mawakili wa Balochistan ameuawa mapema leo kwa kufyatuliwa risasi na watu wasiojulikana katika mji wa Quetta.
Sarfaraz Bugti, Waziri wa Mambo ya Ndani wa eneo la Balochistan amelaumu utepetevu wa maafisa usalama na vyombo vya kiintelijinsia kwa hujuma hiyo ya bomu hospitalini.
Hadi tunaenda mitamboni, hakuna kundi lolote lililokuwa limekiri kuhusika na shambulizi hilo wala mauaji ya wakili mashuhuri katika eneo hilo Sarfaraz Bugti.
Mwishoni mwa mwezi Machi mwa huu, watu 52 waliuawa na makumi ya wengine kujeruhiwa kwenye mlipuko wa bomu uliotikisa mji wa Lahore, kaskazini mashariki mwa Pakistan.
Polisi ya Pakistan ilisema mlipuko huo ulitokea nje ya Bustani ya Gulshan Iqbal mjini Lahore, katika mkoa wa Punjab, ambao ni moja ya mikoa salama isiyoshuhudia hujuma za kigaidi.