Mwanajudo wa Misri akataa kumpa mkono Mzayuni
Huwenda mwanamichezo wa judo raia wa Misri akaadhibiwa kwa kukataa kumpa mkono mpinzani wake raia wa utawala haramu wa Israel katika mashindano ya Olimpiki yanayoendelea huko Rio de Janeiro nchini Brazil.
Msemaji wa Shirikisho la Kimataifa la Judo, Nicolas Messner amesema kuwa, kitendo cha mwanamichezo Islam El Shehaby wa Misri kususia kumpa mkono Or Sasson raia wa Israel aliyekuwa mpinzani wake katika mchezo huo, kitafuatiliwa kwa lengo la kutoa adhabu dhidi yake.
El Shehaby ambaye anatajwa kuwa mpinzani mkubwa dhidi ya utawala wa Kizayuni wa Israel, alisusia kumpa mkono raia huyo wa Kizayuni kutokana kwamba kufanya hivyo ni sawa na kutoa heshima kwa utawala katili wa Israel. Islam El Shehaby alikutana na Or Sasson katika mashindano ya judo ya uzani wa kilogramu 100.
Duru ya 31 ya mashindano ya michezo ya Olimpiki mjini Rio de Janeiro, nchini Brazil ilianza tarehe sita mwezi huu ikiwashirikisha wanamichezo elfu 10 na 444 kutoka nchi mbalimbali za dunia. Mashindano hayo yatafikia tamati tarehe 21 ya mwezi huu.