Ugaidi wa ndani nchini Marekani na mtazamo wa undumakuwili wa Washington
https://parstoday.ir/sw/news/world-i135934-ugaidi_wa_ndani_nchini_marekani_na_mtazamo_wa_undumakuwili_wa_washington
Waziri wa Usalama wa Ndani wa Marekani ametaja aina yoyote ya uchochezi au utekelezaji wa vurugu dhidi ya serikali kuwa ni mfano wa ‘ugaidi wa ndani’.
(last modified 2026-01-27T02:32:39+00:00 )
Jan 27, 2026 02:32 UTC
  • Ugaidi wa ndani nchini Marekani na mtazamo wa undumakuwili wa Washington

Waziri wa Usalama wa Ndani wa Marekani ametaja aina yoyote ya uchochezi au utekelezaji wa vurugu dhidi ya serikali kuwa ni mfano wa ‘ugaidi wa ndani’.

Kwa mujibu wa taarifa ya Pars Today, Kristi Noem, Waziri wa Usalama wa Ndani wa Marekani, alimwelezea kijana aliyekuwa akipinga serikali, na ambaye aliuawa na maafisa wa Idara ya Uhamiaji, kama “gaidi”. Aidha, alisisitiza kuwa aina yoyote ya uchochezi au utekelezaji wa vurugu dhidi ya serikali inaweza kutafsiriwa kama “ugaidi wa ndani”.

Baada ya kuuawa kwa muuguzi aliyekuwa akipinga sera za uhamiaji za Trump kwa kupigwa risasi na maafisa wa Idara ya Uhamiaji na Forodha ya Marekani (ICE), Kristi Noem alitaja hatua za mwanamke huyo kama “ugaidi wa ndani”. Aidha, alimshutumu Tim Walz, Gavana wa Minnesota, na Jacob Frey, Meya wa Minneapolis, kwa kuchochea vurugu dhidi ya maafisa wa shirikisho. Waziri wa Usalama wa Ndani wa Marekani pia alionya kwamba Trump yuko tayari kutekeleza “Sheria ya Uasi” endapo itaonekana kuwa ni lazima.

Alipoulizwa na mwandishi wa habari, ambaye alikumbusha kwamba Ikulu ya White House imemwelezea mtu aliyeuawa kuwa “gaidi wa ndani”, iwapo anakubaliana na tafsiri hiyo na kama kuna ushahidi, alijibu kwa kusema: “Pale ambapo mtu anachochea au kutekeleza vurugu dhidi ya serikali kwa sababu za kiitikadi, na kuendelea kushikilia msimamo huo wa vurugu, hiyo ndiyo tafsiri ya ugaidi wa ndani.”

Waziri wa Usalama wa Ndani wa Marekani kisha akadai kuwa “mtu huyo alikuja akiwa na silaha na risasi kwa lengo la kuzuia maafisa wa uhamiaji kutekeleza sheria”, na akaongeza: “Ametenda kitendo cha ugaidi wa ndani.”

Kauli hizi za Noem zimetolewa ilhali katika video zilizorekodiwa na wananchi waliokuwepo eneo la tukio, Alex Prity, aliyepigwa risasi na kuuawa, anaonekana akiwa na simu mkononi. Katika picha hizo, hakuna sehemu yoyote inayoonyesha wazi kwamba alikuwa ameshika silaha.

Mtazamo wa undumakuwili wa Washington kuhusu suala la ugaidi wa ndani umejadiliwa kwa miaka mingi katika uchambuzi wa kisiasa na taarifa za vyombo vya habari. Hoja hii ilijitokeza kwa uwazi zaidi pale Waziri wa Usalama wa Ndani wa Marekani alipotangaza kwamba kila aina ya vurugu dhidi ya maafisa wa shirikisho au taasisi za serikali inaweza kuchukuliwa kama “ugaidi wa ndani”. Msimamo huu unaweza kueleweka ndani ya mfumo wa sheria za Marekani, kwa kuwa serikali ya shirikisho daima huwatetea maafisa wake, na suala hilo hutazamwa kama mstari mwekundu. Hata hivyo, tafsiri hii inapotumika nje ya Marekani, hupimwa kwa vigezo tofauti kabisa, na tofauti hiyo ndiyo inayoibua mjadala kuhusu mtazamo wa undumakuwili wa Washington.

Katika miaka ya hivi karibuni, hasa baada ya machafuko ya Januari 2026 nchini Iran, Marekani imekuwa ikikosoa hatua za vyombo vya usalama vya Iran dhidi ya watu ambao, wakati wa ghasia, walitumia silaha za moto, silaha za jadi, kuchoma mali ya umma au kushambulia maafisa wa polisi. Katika simulizi rasmi ya Washington, vitendo hivi vya wahalifu hutajwa kama “maandamano ya wananchi”, na majibu ya vyombo vya usalama vya Iran huitwa “ukandamizaji”.

Huku Marekani ikitoa tafsiri hiyo kwa matukio ya nje, ndani ya mipaka yake hata shambulio dhidi ya majengo ya serikali, uharibifu wa mali ya umma au vitisho dhidi ya polisi na maafisa wa kutekeleza sheria, kama maafisa wa uhamiaji, huainishwa bila kusita kama vitendo vya vurugu, na kwa sasa, kama ugaidi wa ndani.

Mfano ulio wazi wa mkinzano huu unaweza kuonekana katika namna serikali ya Marekani ilivyokabiliana na shambulio la tarehe 6 Januari 2021 dhidi ya jengo la Bunge. Katika tukio hilo, kundi la waandamanaji walioingia katika maeneo ya serikali walikabiliwa na hatua kali za kisheria na kiusalama, na wengi wao walishtakiwa kwa makosa mazito, ikiwemo “kufanya vitendo dhidi ya serikali”.

Magaidi wanaopata himaya ya Marekani na Israel wakiteketeza mali ya umma nchini Iran

Katika muktadha huohuo, Waziri wa Usalama wa Ndani wa Marekani alisisitiza kwamba aina yoyote ya vurugu dhidi ya taasisi za serikali ni tishio kwa usalama wa taifa na lazima ikabiliwe kwa hatua kali. Msimamo huu unaonyesha kwamba, katika mtazamo wa Washington, usalama wa taasisi za dola na maafisa wa shirikisho ni mstari mwekundu ambao kuvukwa kwake kunakabiliwa na majibu makubwa na yasiyo na muhula.

Lakini vigezo hivi hivi vinapohusishwa na Iran, tafsiri hubadilika. Katika ripoti na taarifa rasmi za Marekani, hata makundi yaliyoshambulia polisi, kutumia silaha za moto au kuharibu mali ya umma bado huwasilishwa kama “waandamanaji”.

Hii ni licha ya ukweli kwamba katika sheria za nchi nyingi, ikiwemo Marekani, tabia kama hizi hutambuliwa waziwazi kama vitendo vya vurugu vilivyoratibiwa au hatua dhidi ya usalama wa jamii. Wataalamu na wachambuzi wanaamini kwamba tofauti hii katika namna simulizi zinavyojengwa haitokani na tofauti katika asili ya matendo, bali ni matokeo ya mtazamo wa unafiki au undumakuwili wa Washington kuhusu suala la ugaidi.

Kutokana na mtazamo wa kisheria, inawezekana pia kuchunguza mkinzano huu. Ndani ya Marekani, serikali hutumia nyenzo mbalimbali, kama sheria za kupambana na ugaidi, mifumo ya uangalizi wa kiusalama na mashitaka ya mahakamani, ili kukabiliana na vitisho vya usalama. Lakini katika sera za nje, hatua kama hizi zinapotekelezwa na nchi nyingine, hasa zile zinazokataa kusalimu amri mbele ya matakwa ya Marekani, mara nyingi hutajwa kama ukiukaji wa haki za binadamu. Tofauti hii ya vigezo, kwa mara nyingine, inazua maswali makubwa kuhusu viwango vinavyotumiwa na Marekani inapozungumzia ugaidi.

Hatimaye, hoja kuu ni hii: ikiwa vurugu dhidi ya maafisa wa serikali ya shirikisho nchini Marekani hutambuliwa kama “ugaidi wa ndani”, basi kwa nini kukabiliana na watu au makundi yenye silaha au yanayofanya vitendo vya vurugu katika nchi nyingine, hasa Iran, hupimwa kwa vigezo tofauti na hata kulaaniwa kama ukandamizaji? Je, inawezekana kitendo kimoja kifanyike katika nchi mbili tofauti lakini kielezwe kwa maneno mawili yanayopingana kabisa, na bado kudai kuwa kuna utiifu kwa kanuni zisizobadilika na zilizo wazi kuhusu ugaidi?