Jun 22, 2022 01:16 UTC
  • Jumatano tarehe 22 Juni mwaka 2022

Leo ni Jumatano tarehe 22 Dhulqaada 1443 Hijria sawa na Juni 22 mwaka 2022.

Siku kama ya leo miaka 1035 iliyopita yaani tarehe 22 Dhulqaada mwaka 408 Hijria Qamaria, alizaliwa Khoja Nizam al-Mulk, msomi na shakhsia muhimu wa kisiasa na kiutamaduni wa karne ya tano Hijiria mjini Tus, moja ya miji ya kaskazini mashariki mwa Iran. Nizam al-Mulk alikuwa mmoja wa wasomi ambao walikuwa na taathira kubwa katika mabadiliko ya kisiasa na kiutamaduni katika karne hizo. Katika kipindi cha silsila ya utawala wa Masaljuki, Khoja Nizam al-Mulk aliteuliwa kushika wadhifa wa uwaziri ambapo aliendelea kujishughulisha na masuala ya uongozi kwa kipindi cha miaka 30 na kufanikiwa kuiletea Iran ya wakati huo, maendeleo makubwa hususan katika uga wa utamaduni.

Miaka 907 iliyopita katika siku kama ya leo  yaani tarehe 22 Dhulqaada mwaka 536 Hijria Qamaria, kazi ya kuandika tafsiri mashuhuri ya Majmaul Bayan ilimalizika. Kitabu hicho kiliandikwa na Sheikh Tabarsi mmoja wa wafasiri wakubwa wa Qur'ani Tukufu na miongoni mwa maulamaa mashuhuri wa Iran aliyekuwa mashuhuri kwa jina la Aminul Islam kutokana na uaminifu na uchamungu wake. Kitabu hicho ni miongoni mwa tafsiri mashuhuri za Qur'ani kutokana na mbinu yake ya kuvutia katika mtazamo wa fasihi. Tafsiri hiyo imechapishwa mara kadhaa katika nchi za Iran, Lebanon na Misri.

Tafsiri ya Qur'ani ya Majmaul Bayan

Miaka 389 iliyopita mnajimu, mtaalamu wa hisabati na mwanafizikia wa Italia Galileo Galilei alilazimika kukana itikadi zake za kisayansi na kielimu mbele ya viongozi wa Kanisa. Mwaka 1632 Galilei aliandika kitabu akijibu na kukosoa mitazamo ya Betlemosi kuhusu sayari ya jua na kutangaza kuwa dunia inazunguma jua. Mwaka mmoja baadaye Papa wa Kanisa Katoliki alimwita Galileo mjini Roma na kuitaja mitazamo hiyo ya kisayansi kuwa ukafiri. Kwa msingi huo, kanisa lilimlazimisha Galileo akane itikadi zake za kielimu la sivyo akabiliwe na adhabu ya kifo. Japokuwa msomi huyo alikana mitazamo yake hiyo ya kielimu kidhahiri tu lakini wakati alipotoka nje ya mahakama alipiga chini mguu wake na kuiambia ardhi: "Licha ya haya yote lakini wewe unazunguka."

Galileo Galilei

Siku kama ya leo miaka 81 iliyopita, katika Vita vya Pili vya Dunia, jeshi la Ujerumani ya Kinazi lilianza mashambulizi makubwa dhidi ya Urusi ya zamani kwa jina la Operesheni ya Barbarossa. Kwa utaratibu huo Adolph Hitler akaanzisha vita vingine katika upande wa mashariki mwa Ujerumani kwa shabaha ya kutimiza mipango yake ya kutaka kujitanua zaidi. Hadi wakati huo tayari dikteta huyo alikuwa ameteka nchi kadhaa za Ulaya.

Operesheni ya Barbarossa

Katika operesheni hiyo, askari wa Ujerumani walisonga mbele na kufika katika viunga vya mji mkuu wa nchi hiyo, Moscow. Hata hivyo jeshi la Ujerumani lilipata matatizo makubwa kufuatia kuanza kipindi cha baridi kali na hivyo likashindwa kusonga mbele. Wananchi na jeshi la Urusi katika miji mbalimbali ya nchi hiyo hususan Moscow, Leningrad na Stalingrad walipambana vikali na jeshi hilo vamizi na kulilazimisha kurudi nyuma. Mwezi Agosti 1944 jeshi la Urusi lilifika katika mipaka ya Ujerumani.

Katika siku kama ya leo miaka 47 iliyopita ilianzishwa Harakati ya Ukombozi wa Chad. Tangu mwishoni mwa karne ya 19 nchi ya Chad iliyoko katikati mwa Afrika ilikuwa chini ya udhibiti wa Ufaransa na ilipata uhuru mwaka 1960 baada ya kukoloniwa kwa kipindi cha karibu miaka 80. Hata hiyo iligawanyika katika sehemu mbili tofauti. Sehemu ya kaskazini iliyokuwa nyuma kimaendeleo na kiuchumi, na ya kusini iliyokuwa na suhula nyingi na makau makuu ya nchi ambayo ilidhibitiwa na Wakristo. Tarehe 22 Juni mwaka 1960 kuliundwa Chama cha Maendeleo ya Chad kwa lengo la kuunganisha tena nchi hiyo na kuimarisha umoja wa kitaifa na ustawi wa kiuchumi. Chama hicho kilivunjwa mwaka 1973 na nafasi yake ikachukliwa na Harakati ya Kitaifa ya Mapinduzi ya Kiutamaduni na Kijamii.

Bendera ya Chad

 

 Na miaka 41 iliyopita sawa na tarehe Mosi Tir mwaka 1360 kwa mujibu wa Kalenda ya Kiirani, hayati Imam Ruhullah Khomeini alipasisha uamuzi wa Bunge la Jamhuri ya Kiislamu wa kutokuwa na imani na rais wa wakati huo Abul Hassan Bani Sadr na kwa utaratibu huo kiongozi huyo akalazimika kung'atuka madarakani. Bani Sadr ni miongoni mwa watu waliojidhihirisha kuwa wapenzi na watetezi wa harakati za Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran baada ya Imam Khomeini kuhamia Paris, Ufaransa na alifanikiwa kushika madaraka ya nchi na kuwa rais katika uchaguzi wa kwanza wa baada ya Mapinduzi ya Kiislamu nchini kwa kutumia ujanja wa kipropaganda. Muda mfupi baadaye Imam Khomeini alimkabidhi ukamanda wa majeshi ya Jamhuri ya Kiislamu. Hata hivyo Bani Sadr aliyekuwa mtu mwenye uchu wa madaraka, mwenye kiburi na msaliti alianza mara moja kushirikiana na makundi yaliyokuwa yakipinga Mapinduzi ya Kiislamu kwa lengo la kuangusha utawala wa Kiislamu nchini Iran.

Abul Hassan Bani Sadr