Apr 21, 2024 07:57 UTC
  • Zaidi ya watu 50 wamepoteza maisha baada ya boti kupinduka Jamhuri ya Afrika ya Kati

Takriban watu 58 waliokuwa wakienda mazishini wameaga dunia baada ya boti yao kupinduka majini katika mji mkuu wa Jamhuri ya Afrika ya Kati, Bangui. Haya yalielezwa jana na mkuu wa ulinzi wa raia.

Tuliweza kutoa miili 58 kutoka mtoni hata hivyo hatujui idadi ya watu ambao wako chini ya maji. Amesema Thomas Djimasse mkuu wa ulinzi wa raia. Watu walioshuhudia boti hiyo ikizama huko Bangui mji mkuu wa Jamhuri ya Afrika ya Kati pamoja na picha za video zilizosambazwa katika mitandao ya kijamii zinaonyesha kuwa boti hiyo iliyozama ilikuwa imepakia watu zaidi ya 300; wengine wakiwa wamesimama na wengine wamesongamana ndani ya boti hiyo. Walikuwa wakielekea katika mazishi ya mkuu wa kijiji wakati ilipopinduka katika Mto Mpoko. 

Jamhuri ya Afrika ya Kati 

Timu ya uokoaji ilifika sehemu ya tukio dakika 40 baada ya boti kupinduka. Maurice Kapenya ambaye alikuwa akiisindikiza boti hiyo kwa mtumbwi kwa sababu hakukuwa na nafasi ndani ya boti hiyo amesema kuwa aliikusanya miili ya baadhi ya wahanga akiwemo dada yake kwa kusaidiwa na wavuvi na wenyeji. 

Familia mbalimbali jana zilionekana kuwasaka wapendwa wao ambao wanaaminika kuwa wako ndani ya maji. Majeruhi wa ajali hiyo ya kuzama boti wako hospitali wakiendelea kupata matibabu.  

Kujaza watu kupindukia imetajwa kuwa sababu ya ajali hiyo ya boti.  

 

Tags