Askari wa AU nchini Somalia wafungwa jela kwa kufanya ulaghai
Askari tisa wa Kikosi cha Kulinda Amani cha Umoja wa Afrika nchini Somalia AMISOM wamehukumiwa vifungo jela kwa kuendesha biashara ya ulaghai ya mafuta katika nchi hiyo ya Pembe ya Afrika.
Taarifa ya AMISOM imesema kuwa, askari hao wote wa Uganda, wakiwemo mameja wawili, wamehukumiwa vifungo vya kati ya mwaka mmoja na mitatu jela baada ya kupatikana na hatia na mahakama ya kijeshi ya Kampala ya kufanya biashara haramu ya mafuta nchini Somalia.
Hii ni mara ya kwanza kwa korti ya kijeshi kuketi na kutoa hukumu dhidi ya askari wa kulinda amani wa AU, tangu kikosi cha AMISOM kitumwe nchini Somalia miaka tisa iliyopita.
Mapema mwezi Juni mwaka huu, AMISOM ilisema imekamata na kuwazuilia askari wake watano wanaotuhumiwa kuuza kinyume cha sheria suhula na bidhaa za kikosi hicho. Taarifa ya AMISOM ilisema kuwa, askari hao walipatikana na fueli na mifuko ya kikosi hicho kinyume cha sheria, baada ya kukamatwa katika operesheni ya pamoja iliyohusisha kikosi hicho na polisi ya Somalia.
Askari elfu 22 wa Afrika aghalabu yao kutoka Uganda walitumwa nchini Somalia miaka 9 iliyopita kwa ajili ya kurejesha amani na kukabiliana na harakati za kundi la kigaidi la al-Shabaab.
Mbali na tuhuma za wizi, askari wa kulinda amani katika nchi nyingi duniani na haswa za Kiafrika kama vile Jamhuri ya Afrika ya Kati, wamekuwa wakikabiliwa pia na madai ya ubakaji.