Wanadiplomasia wa Baraza la Usalama kuelekea Sudan Kusini
Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Sudan Kusini amesema leo kuwa wanadiplomasia wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa watafanya ziara nchini humo siku chache zijazo.
Mawien Makol Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Sudan Kusini amesema kuwa tarehe rasmi ya kufanyika safari hiyo ya wanadiplomasia wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa nchini humo bado haijawekwa wazi, lakini akasema hadi kufikia kesho kutwa tarehe ya kufanyika ziara hiyo itatangazwa.
Ellen Margrethe Loej Mkuu wa kikosi cha kulinda amani cha Umoja wa Mataifa nchini Sudan Kusini (UNMISS) alisema Jumanne baada ya kufanya mazungumzo na Deng Alor Waziri wa Mambo ya Nje wa Sudan Kusini kuwa atashirikiana na serikali na waziri huyo wa Mambo ya Nje ili kuandaa uwanja wa kufanyika mazungumzo kati ya wanachama wa Baraza la Usalama, Rais na viongozi wa serikali ya Juba.
Kuongezeka mapigano huko Juba mji mkuu wa Sudan Kusini kumezidisha wasiwasi kuhusu uwezekano wa kutokea vita vya ndani na kuulazimu Umoja wa Mataifa kutuma wanajeshi zaidi nchini humo.