Wapinzani Gabon waomba msaada wa kimataifa
-
Jean Ping, Waziri wa zamani wa Mambo ya Nje wa Gabon
Kiongozi wa upinzani Gabon huko katikati mwa Afrika ameomba msaada wa kimataifa ili kusaidia kuwalinda raia nchini humo kufuatia shambulio lililofanywa na vikosi vya serikali kwenye makao makuu ya wapinzani huko Libreville mji mkuu wa nchi hiyo, baada ya kutangazwa matokeo ya uchaguzi wa Rais yaliyopingwa na wapinzani.
Jean Ping, Waziri wa zamani wa Mambo ya Nje wa Gabon na ambaye sasa ni kiongozi wa upinzani amesema leo kuwa, wananchi wa Gabon wapo hatarini na kwamba jamii ya kimataifa inapaswa kwenda nchini humo kuwasaidia raia.
Ali Bongo ambaye amekuwa madarakani Gabon tangu kufanyika uchaguzi uliozua mivutano mwaka 2009 jana alitangazwa rasmi kuwa mshindi wa uchaguzi wa Rais wa hivi karibuni nchini humo. Ping na wagombea wengine wamepinga matokeo ya uchaguzi huo.
Jean Ping amesema kuwa kila mmoja anafahamu kuwa yeye ndiye mshindi halisi wa uchaguzi wa Rais wa Gabon uliofanyika Jumamosi iliyopita. Wafuasi wa Ping jana usiku walichoma moto bunge la taifa huko Libreville masaa machache baada ya Ali Bongo kutangazwa kuwa mshindi wa kiti cha urais.