UN: Jeshi la Sudan Kusini ndilo linaloongoza machafuko yanayojiri nchini humo
Umoja wa Mataifa umesema jeshi la Sudan Kusini lina mkono katika machafuko yanayojiri nchini humo.
Kupitia ripoti yake, Umoja wa Mataifa umeashiria hali mbaya ya kibinadamu ambayo imeshuhudiwa nchini Sudan Kusini katika miezi ya hivi karibuni na kutangaza kuwa uongozi wa jeshi la Sudan Kusini uliongoza mapigano yaliyotokea mwezi Julai nchini humo.
Ripoti ya Umoja wa Mataifa imefafanua kuwa machafuko na ukatili ambao haujawahi kushuhudiwa uliotokea mwezi Julai, ukiwemo uporaji na ubakaji wa halaiki haukufanywa na askari tu waliojichukulia hatua mikononi mwao.
Wimbi jipya la mapigano nchini Sudan Kusini lilizuka mwezi Julai baina ya vikosi vitiifu kwa Rais Salva Kiir na wafuasi wa aliyekuwa makamu wake Riek Machar ambaye sasa ni kiongozi wa waasi.
Kushtadi mapigano na machafuko Sudan Kusini kumehatarisha makubaliano tete ya amani yaliyofikiwa mwaka uliopita kwa madhumuni ya kuhitimisha miezi 18 ya vita vya wenyewe kwa wenyewe.
Maelfu ya watu wameuawa na kujeruhiwa tangu ulipoanza mgogoro nchini Sudan Kusini mwaka 2013.
Aidha raia wapatao milioni nne na laki nane wa nchi hiyo changa zaidi barani Afrika, ambao ni sawa na takribani nusu ya watu wote wa nchi hiyo wanakabiliwa na uhaba mkubwa wa chakula.../