Majeshi ya Niger, Chad yaua magaidi 38 wa Boko Haram
Majeshi ya Niger na Chad yameua magaidi 38 wa kundi la kitakfiri la Boko Haram katika miji miwili ya mpakani kusini mashariki mwa Niger mapema wiki hii.
Wanajeshi wawili kutoka kikosi cha pamoja cha nchi hizo mbili walijeruhiwa katika oparesheni hiyo ilianzishwa kufuatia mapigano katika kijiji cha Toumour karibu na eneo la Ziwa Chad na mpaka wa Nigeria.
Wanajeshi wa Niger na Chad pia walifanikiwa kuteka kiasi kikubwa cha silaha za magaidi hao wa Boko Haram ambao bado wanasakwa na vikosi hivyo.
Tokea Boko Haram ianzishe uasi wake Nigeria mwaka 2009, watu elfu 20 wamepoteza maisha. Aidha zaidi ya watu milioni mbili wamefanywa wakimbizi kufuatia ugaidi wa Boko Haram.
Neno Boko Haram kwa lugha ya Kihausa lina maana ya 'elimu kutoka nchi za Magharibi ni haramu'. Kundi hilo la Boko Haram ambalo lina ufahamu usio sahihi na potofu kuhusu dini ya Kiislamu, limekuwa likifanya hujuma katika maeneo mbalimbali ya Nigeria hasa kaskazini mashariki mwa nchi hiyo.