UN: Nigeria inakabiliwa na hali mbaya zaidi ya kibinadamu barani Afrika
Kaimu Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa anayehusika na uratibu wa misaada ya kibinadamu ameonya kuwa Nigeria ni nchi inayokabiliwa na hali mbaya zaidi ya kibinadamu barani Afrika ambapo watoto wapatao 400,000 wanataabika kwa njaa huku raia wakiteseka kwa kupata kiwango kidogo au kukosa kabisa ulinzi, usalama, chakula au hata maji safi.
Peter Lundberg ameeleza hayo kupitia taarifa iliyotolewa jana na Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Uratibu wa Misaada ya Kibinadamu (OCHA). Aidha ameihakikishia serikali ya Nigeria kuwa jamii ya kimatatifa inaahidi kufanya kazi kwa karibu na vyombo vya serikali ya shirikisho na serikali za majimbo za nchi hiyo ili kuongeza kasi ya uchukuaji hatua za kukabiliana na hali hiyo.
Licha ya baadhi ya hatua nzuri zilizochukuliwa kupitia Mfuko Mkuu wa Dharura wa Uchukuaji Hatua wa Umoja wa Mataifa (CERF) pamoja na jamii ya wafadhili, Mpango wa Hatua za Kibinadamu wa Nigeria kwa mwaka 2016 ambao unahitaji jumla ya dola milioni 484, hadi sasa umepokea thuluthi moja tu ya fedha hizo.
"Bila ya kuwepo nyenzo za utekelezaji, watoto wadogo wa kiume na wa kike, wanawake na wanaume watafariki dunia. Mahitaji ya kipaumbele cha kwanza unabaki kuwa ni usalama wa chakula ambapo ni asilimia 25 tu ya fedha zimechangiwa hadi sasa" ameonya Lundberg…/