Waziri apigwa kalamu nyekundu Tunisia kwa kukosoa Uwahabi
Serikali ya Tunisia imemfuta kazi Waziri wa Masuala ya Dini wa nchi hiyo, baada ya kusema kuwa, idiolojia ya Uwahabi ambayo imetawala Saudi Arabia ndiyo chanzo cha ugaidi duniani.
Taarifa ya serikali ya Tunis imesema kuwa, Yousuf Shahid, Waziri Mkuu wa nchi hiyo ya Kiafrika amempiga kalamu nyekundu Abdul Jalil Bin Salim, kwa kile kinachodaiwa kuwa 'ameshambulia misingi ya udiplomasia'.
Hapo jana, Abdul Jalil Salim alikiambia kikao cha Kamisheni ya Haki, Uhuru na Uhusiano wa Kigeni ya Bunge la Tunisia kwamba, mfumo wa Saudi Arabia unazalisha ugaidi na misimamo mikali.
Waziri wa Masuala ya Dini wa Tunisia aliwataka viongozi wa Saudi Arabia kurekebisha siasa zao ambazo amesisitiza kuwa lengo lake kuu ni kutengeneza watu wenye misimamo mikali na magaidi.
Waziri huyo aliyepigwa kalamu alifafanua kuwa, fikra za kuwakufurisha Waislamu wengine hazipatikani katika madhehebu yoyote ya Kiislamu isipokuwa madhehebu ya Kihanbali na kundi la Kiwahabi na kwamba historia inathibitisha kuwa ugaidi ni zao lililotokana na fikra za kidini za Suadia.
Kadhalika Abdul Jalil Bin Salim amewahi kunukuliwa na idhaa moja ya kibinafsi ya Mosaique FM akiitaka Saudia kufanya mageuzi katika vyuo vyake akisisitiza kuwa ugaidi kihistoria umezaliwa vyuoni hapo.