Zuma ampiga kalamu nyekundu Waziri wa Fedha wa Afrika Kusini
Rais Jacob Zuma wa Afrika Kusini amempiga kalamu nyekundu Waziri wa Fedha wa nchi hiyo, Pravin Jamnadas Gordhan.
Rais Zuma amechukua uamuzi huo ikiwa ni baada ya siku kadhaa kuenea tetesi ya kudorora soko la nchi hiyo. Tetesi hizo zlikuja kufuatia amri ya Rais Zuma ya kuvunja safari ya Pravin Jamnadas Gordhan ya Marekani na Uingereza kwa ajili ya kuvutia uwekezaji na kutia saini mikataba ya kibiashara na kiuchumi na viongozi wa nchi hizo.
Taarifa iliyotolewa na Ikulu ya Rais imesema kuwa, Gordhan amefutwa kazi na nafasi yake kuchukuliwa na Malusi Nkanyezi Gigaba. Kadhalika Rais Jacob Zuma amemfuta kazi Naibu Waziri wa Fedha, Mcebisi Jonas na nafasi yake kuchukuliwa na Sifiso Buthelezi.
Hayo yanajiri katika hali ambayo, vyama vingi vya siasa kikiwemo chama cha kikomonisti chenye ushirika na chama tawala nchini Afrika Kusini, vimekosoa uamuzi wa Rais Zuma wa kumfuta kazi Pravin Jamnadas Gordhan na kuitaja hatua hiyo kuwa ni ya kidikteta.