Kiongozi wa upinzani wa Afrika Kusini azuiwa kuingia nchini Zambia
Viongozi wa serikali nchini Zambia wamemzuia kuingia nchini humo kiongozi wa upinzani wa Afrika Kusini.
Taarifa zinaeleza kuwa, polisi nchini Zambia jana walimzuia Mmusi Maimane kiongozi wa chama kikuu cha upinzani nchini Afrika Kusini cha Democratic Alliance kuingia nchini humo.
Mmusi Maimane mkuu wa chama cha Democratic Alliance, alikuwa akitarajiwa kuhudhuria kesi inayomkabili kiongozi wa upinzani nchini Zambia Haikande Hichilema.
Duru za karibu na serikali ya Zambia zinasema kuwa, kiongozi huyo wa upinzani wa Afrika Kusini alizuiwa kuingia nchini humo kutokana na hatua yake ya kumuunga mkono kiongozi wa upinzani nchini Zambia Haikande Hichilema ambaye anakabiliwa na kesi ya uhaini.
Kiongozi huyo wa upinzani wa Afrika kusini Mmusi Maimane amesema kuwa, amelazimika kurudi nyumbani baada ya maafisa wa usalama kuingia ndani ya ndege ya Shirika la Ndege la Afrika Kusini aliyokuwa amesafiria mjini Lusaka, kumvamia na kumnyang'anya simu yake na kutomruhusu kuingia nchini humo.
Hakainde Hichilema kiongozi wa upinzani aliyewania kiti cha urais katika uchaguzi uliopita na kutoa ipinzani mkali kwa Rais Edgar Lungu ameshtakiwa kwa makosa ya uhaini. Maimane amekuwa akimtetea Hichilema na kusisitiza kwamba, tuhuma dhidi ya mwanasiasa huyo zina matashi ya kisiasa.