Baraza la Usalama lataka kufanyika uchaguzi wa Rais Kongo
Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa limeitaka serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo ichukue hatua ya kuhakikisha kuwa uchaguzi wa Rais unafanyika nchini humo hadi kufikia mwishoni mwa mwaka huu.
Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa limeeleza kutiwa wasiwasi na mwenendo wa kinyonga wa makubaliano yaliyofikiwa nchini humo kwa ajili ya kuendesha uchaguzi wa Rais na kutahadharisha kuwa kushindwa kutekelezwa muafaka huo kutazidisha hatari ya machafuko na ukosefu wa amani nchini humo na katika eneo zima kwa ujumla.
Mkuu wa Tume ya Uchaguzi ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo tarehe 7 mwezi huu alitangaza kuwa haiwezekani uchaguzi wa rais wa nchi hiyo ukafanyika hadi kufikia mwezi Disemba mwaka huu. Mgogoro wa kisiasa nchini Kongo ulianza kufuatia kuakhirishwa tarehe ya kufanyika uchaguzi wa Rais na vile vile sisitizo la Rais Joseph Kabila la kusalia madarakani.
Inaonekana kuwa ni jambo lisilowezekana kufanyika uchaguzi wa Rais huko Kongo licha ya makubaliano yaliyofikiwa kati ya wapinzani na serikali ya Kinshasa ambayo yaliainisha tarehe 31 Disemba kuwa siku ya kufanyika uchaguzi wa Rais.