ANC yapinga wito wa kuvunjwa Bunge Afrika Kusini
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i33002-anc_yapinga_wito_wa_kuvunjwa_bunge_afrika_kusini
Chama tawala nchini Afrika Kusini cha African National Congress (ANC) kimepinga wito wa kuvunjwa Bunge la nchi hiyo.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
Aug 11, 2017 11:23 UTC
  • ANC yapinga wito wa kuvunjwa Bunge Afrika Kusini

Chama tawala nchini Afrika Kusini cha African National Congress (ANC) kimepinga wito wa kuvunjwa Bunge la nchi hiyo.

Msemaji wa ANC, Nonceba Mhlauli amepinga wito uliotolewa na chama cha upinzani cha Democratic Alliance (DA) wa kuvunjwa Bunge la nchi hiyo kwa shabaha ya kutayarisha mazingira ya kuitishwa uchaguzi mkuu wa mapema na kusema ni mbinu ya kutaka kubadilisha utawala wa nchi hiyo.

Nonceba Mhlauli amesisitiza kuwa wito wa kupiga kura ya kutokuwa na imani na serikali ya Rais Jacob Zuma unaoendelea kutolewa na chama cha Democratic Alliance unapingana na misingi ya demokrasia na kupuuza matakwa ya wananchi.

Bunge la Afrika Kusini

Alkhamisi iliyopita muungano wa DA unaoundwa na vyama vitatu vya upinzani uliwasilisha bungeni muswada wa kura ya kutokuwa na imani na Rais Jacob Zuma wa Afrika Kusini ambao ulishindwa kupata kura za kutosha. 

Hiyo ilikuwa mara ya saba kwa Rais Zuma kunusurika shoka hilo la Bunge la Afrika Kusini. Zuma anakabniliwa na tuhuma za ufisadi na kutumia vibaya madaraka yake.