Mafuriko yaua watu 10 Kongo DR, 90 watoweka
Watu wasiopungua 10 wamepoteza maisha baada ya kusombwa na mafuriko mashariki mwa Jamhuri mwa Kidemokrasia ya Kongo.
Kadhalika watu zaidi ya 90 wameripotiwa kutoweka kutokana na mafuriko hayo.
Dieudonne Tshishiku, afisa wa eneo la Masisi mkoa wa Kivu Kaskazini amesema timu za waokoaji zimetumwa katika mji wa Bihambwe kwenda kuwatafuta manusura na miili ya watu waliosombwa na mafuriko hayo.
Mafuriko hayo ambayo yamevunja kingo za mto ulioko mjini hapo yamesababishwa na mvua kubwa zinazoendelea kunyesha katika nchi hiyo ya Afrika.
Haya yanajiri katika hali ambayo, mlipuko wa ugonjwa wa kipindupindu nchini Jamhuri ya Demokrasia ya Kongo hadi sasa umepelekea watu 528 kupoteza maisha na yumkini mafuriko hayo yakaongeza idadi ya vifo hivyo.
Mripuko wa ugonjwa huo umeathiri miji kadhaa ya mashariki, magharibi, kaskazini na baadhi ya maeneo ya jiji la Kinshasa. Kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani WHO, majimbo 20 kati ya 26 yameathiriwa na ugonjwa huo.