Jeshi Kenya laua waandamanaji watatu, magari kadhaa yachomwa, Raila arejea nchini
Watu watatu wameuawa hii leo wakati jeshi la polisi la Kenya lilipojaribu kutawanya waandamanaji waliokusanyika kupokea msafara wa kiongozi wa upinzani, Raila Odinga aliyerejea nchini mapema leo akitokea nje ya nchi.
Polisi ya Kenya imetumia gesi ya kutoa machozi na kufyatua risasi angani dhidi ya wafuasi wa Odinga waliokuwa katika barabara inayotoka Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Jomo Kenyatta wakielekea mjini kati jijini Nairobi.
Waandamanaji watatu wameuawa katika mapigano yaliyotokea baina yao na polisi waliokuwa wakitaka kuzua waandamanaji hao kuingia katika maeneo ya kibiashara mjini Nairobi. Ripoti zinasema magari kadhaa yameteketezwa kwa moto katika ghasia na machafuko hayo.
Wandamanaji hao walimiminika katika barabara ya Mombasa inayounganisha Uwanja wa Ndege wa Kimataifa Jomo Kenyatta na jiji la Nairobi tangu mapema leo kwa ajili ya kumlaki kiongozi wa upinzani Raila Odinga.
Odinga ametoa wito wa kuanzishwa harakati ya kitaifa ya kupinga matokeo ya uchaguzi wa rais wa marudio uliofanyika mwezi uliopita.
Tume ya Uchaguzi ya Kenya imetangaza kuwa Rais wa sasa wa nchi hiyo, Uhuru Kenyatta, ameshinda uchaguzi huo uliosusiwa na kinara wa upinzani, Raila Odinga kwa kupata asilimia 98 ya kura. Asilimia 39 tu ya raia waliojiandikisha kupiga kura ndio walioshiriki katika zoezi hilo.