Mgomo wa nchi nzima wa wafanyakazi waanza nchini Tunisia
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i50927-mgomo_wa_nchi_nzima_wa_wafanyakazi_waanza_nchini_tunisia
Muungano mkubwa zaidi wa wafanyakazi nchini Tunisia UGTT umesema mgomo wa nchi nzima wa malaki ya watumishi wa umma umeng'oa nanga hii leo Alkhamisi.
(last modified 2026-03-17T04:36:21+00:00 )
Jan 17, 2019 04:10 UTC
  • Mgomo wa nchi nzima wa wafanyakazi waanza nchini Tunisia

Muungano mkubwa zaidi wa wafanyakazi nchini Tunisia UGTT umesema mgomo wa nchi nzima wa malaki ya watumishi wa umma umeng'oa nanga hii leo Alkhamisi.

Mgomo huo ni wa kushinikiza serikali ya Tunis iwape nyongeza ya mishahara wafanyakazi wa umma wapatao laki sita na 70 elfu. Mgomo huo umeathiri zaidi huduma katika viwanja vya ndege, mashule na hata shirika la habari la serikali.

Mgomo huo wa wafanyakazi wa serikali umeanza katika hali ambayo, Tunisia kwa siku kadhaa sasa imekuwa ikishuhudia maandamano ya wananchi wakilalamikia utendaji wa serikali na hali mbaya ya uchumi nchini humo. 

Maandamano ya Vizibao Vyekundu nchini Tunisia

Nchi hiyo iko chini ya mashinikizo ya Mfuko wa Fedha Duniani IMF unaoitaka isimamishe mishahara ya wafanyakazi wa sekta za umma, kama sehemu ya mageuzi ya kujaribu kupunguza nakisi ya bajeti ya nchi.

Nchi wafadhili zimetishia kuacha kuusaidia uchumi wa Tunisia, ambao unayumba na kukabiliwa na mgogoro mkubwa tokeo aondolewe madarakani dikteta wa zamani wa nchi hiyo, Zainul Abiddin Ben Ali mwaka 2011.