Idadi ya waliouawa katika mapigano Libya yafikia watu 32
Idadi ya watu waliouawa katika mapigano kati ya vikosi vya Serikali ya Maafikiano ya Kitaifa na vile vinavyoongozwa na Jenerali Khalifa Haftar nchini Libya imeongezeka na kufikia watu 32.
Hayo yalitangazwa jana usiku na A'hmid Omar, Waziri wa Afya wa Serikali ya Maafikiano ya Kitaifa na kuongeza kuwa, watu wengine 50 wamejeruhiwa katika mapigano hayo.
Vikosi vya Jenerali Khalifa Haftar vimesema vimepoteza askari 14 kufikia sasa, katika mapigano hayo.
Mapigano hayo ambayo yamezusha wasiwasi mkubwa miongoni mwa raia wa Tripoli yamehatarisha juhudi za kieneo na kimataifa za kuupatia ufumbuzi mgogoro wa Libya kupitia njia ya mazungumzo na utatuzi wa kisiasa.
Jenerali Khalifa Haftar ambaye vikosi vyake vinasonga mbele kuelekea mji mkuu Tripoli ametoa ujumbe wa sauti akiwataka wananchi wa Tripoli kutokabiliana na vikosi vyake.
Jamii ya kimataifa imeziasa pande zinazozozana nchini Libya kujizuia na kujiepusha na mashambulizi zaidi.