Wabunge Afrika Kusini wamchagua tena Ramaphosa kuwa rais
Wabunge Afrika Kusini wamemchagua tena Cyril Ramaphosa kuwa rais wa nchi hiyo wiki mbili baada ya chama tawala ANC kushinda katika uchaguzi wa bunge.
Akizungumza na waandishi habari, Jaji Mkuu wa Afrika Kusini Mogoeng Mogoeng amesema Ramaphosa amechaguliwa rasmi kuwa Rais wa Jamhuri ya Afrika Kusini kwani ni jina lake pekee ndilo liliwasilishwa bungeni mjini Cape Town.
Wabunge wa chama tawala cha African National Congress walifanikiwa kushinda viti 230 kati ya 400 katika uchaguzi wa Mei 8 na wamemchagua rais katika kikao chao cha kwanza. ANC ilipata ushindi wa asilimia 57.5 matokeo ambayo yalikuwa mabaya zaidi tokea utawala wa ubaguzi wa rangi uangushwe nchini humo mwaka 1994.
Ramaphosa anatarajiwa kuapishwa Jumamosi na punde baada ya hapo atamteua naibu wa rais na baraza lake la mawaziri.
Kwa mujibu wa katiba ya Afrika Kusini ya mwaka 1996, wabunge waliochaguliwa kupitia kura za moja kwa moja za wananchi ndio humchagua rais wa nchi.