Hatimaye raia wa Kenya aliyesemekana kutekwa nyara Tanzania, apatikana mjini Mombasa
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i54510-hatimaye_raia_wa_kenya_aliyesemekana_kutekwa_nyara_tanzania_apatikana_mjini_mombasa
Mfanyabiashara wa Kenya, Raphael Ongangi anayedaiwa kutekwa nyara na watu wasiojulikana maeneo ya Oysterbay jijini Dar es Salaam Tanzania, amepatikana leo akiwa salama mjini Mombasa nchini Kenya.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
Jul 02, 2019 09:32 UTC
  • Hatimaye raia wa Kenya aliyesemekana kutekwa nyara Tanzania, apatikana mjini Mombasa

Mfanyabiashara wa Kenya, Raphael Ongangi anayedaiwa kutekwa nyara na watu wasiojulikana maeneo ya Oysterbay jijini Dar es Salaam Tanzania, amepatikana leo akiwa salama mjini Mombasa nchini Kenya.

Ongangi anadaiwa kutekwa na watu wasiojulikana tarehe 24 mwezi jana akiwa pamoja na mke wake, Veronica Kundya ambapo inaelezwa kuwa katika tukio hilo walizuiwa na watu hao na kisha kuwatolea silaha aina ya bastola, kuwachukua wote wawili kabla ya kumwachilia huru mkewe na kuondoka na Raphael. Tayari Veronica amethibitisha kupatikana kwa mume wake huyo asubuhi ya leo Jumanne. Kwa mujibu wa mwanamke huyo, mumewe amepatikana  mjini Mombasa nchini Kenya. “Nimezungumza naye mwenyewe yupo Mombasa, tumezungumza kwa kifupi nashukuru sana, mmenisaidia.” Amesema Kundya akilishukuru gazeti la Mwananchi.

Zitto Zuberi Kabwe, Mbunge wa Kigoma Mjini kupitia tiketi ya chama cha ACT- Wazalendo aliyeitaka serikali ya Tanzania kumtafuta Ongangi

Aidha mchana wa leo mwanamke huyo ameandika ujumbe kwenye mtandao wa kijamii unaoelezea kupatikana mume wake kwamba: " Raphael amepatikana Mombasa na yupo salama salimini, sina taarifa nyingine zaidi ya hiyo ila hiyo pia inatosha sana kwangu. Nina haraka sana sitaweza kusema mengi zaidi ya kumshukuru Mungu sana kwa kuwa yeye ni Mungu wa miujiza..." Raphael Ongangi amepatikana ikiwa ni siku moja tangu Zitto Zuberi Kabwe, Mbunge wa Kigoma Mjini kupitia tiketi ya chama cha ACT- Wazalendo nchini Tanzani azungumze na waandishi wa habari kuhusu tukio hilo lililomkuta rafiki yake huyo wa karibu ambaye miaka ya nyuma alikuwa msaidizi wake. Akizungumza jana Zitto aliitaka serikali ya nchi hiyo kuliangalia kwa uzito suala la kutekwa nyara raia huyo wa Kenya anayeishi Tanzania.