Waziri Mkuu wa Ethiopia akadhibisha mauaji ya raia katika eneo la Tigray
Akizungumza katika kikao cha bunge, Abiy Ahmed Waziri Mku wa Ethiopia amekadhibisha kujiri mauaji ya raia katika eneo la Tigray kaskazini mwa nchi hiyo.
Waziri Mkuu wa Ethiopia jana Jumatatu alishiriki katika kikao bungeni ambapo alitoa maelezo kuhusu mashambulizi ya jeshi la nchi hiyo dhidi ya Harakati ya Ukombozi ya Wananchi wa Tigray. Katika kikao hicho, Abiy Ahmed amekadhibisha kuuliwa raia katika eneo hilo na kueleza kuwa harakati ya Tigray People's Liberation Front (TPLF) inafanya njama ya kuvuruga mpango wa kutekeleza mageuzi huko Ethiopia.
Abiy Ahmed ameashiria namna jeshi la nchi hiyo mwanzoni mwa wiki hii lilivyofanikiwa kuudhibiti kikamilifu mji wa Mekelle makao makuu ya jimbo la Tigray na kueleza kuwa, jeshi la Ethiopia halitauharibu wala kuubomoa mji huo licha ya kuudhibiti.
Hii ni katika hali ambayo Harakati ya Ukombozi ya Wananchi wa Tigray inaituhumu serikali kuu ya Addis Ababa kuwa inawalenga raia katika mashambulizi yake ya anga na nchi kavu katika eneo hilo.
Abiy Ahmed Waziri Mkuu wa Ethiopia tarehe 4 mwezi Novemba mwaka huu alitoa amri ya kushambuliwa eneo la Tigray kaskazini mwa nchi hiyo baada ya kuwatuhumu wapiganaji wa harakati ya TPLF kuwa wamevishambulia vikosi vya serikali.