Ulaya yatofautiana na Marekani kuhusu kuwekewa vikwazo DRC
Nchi za bara Ulaya zimetilia shaka hatua ya Marekani kushinikiza kuwekewa vikwazo Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo kwa lengo la kumtaka Rais Joseph Kabila wa nchi hiyo asigombee urais kwa muhula wa tatu.
Serikali ya Washington kupitia Bunge la Seneti na Mjumbe Maalumu wa Marekani katika eneo la Maziwa Makuu barani Afrika, Tom Perriello, inashinikiza kuwekewa vikwazo watu wa karibu na Rais Kabila wakiwemo maafisa serikalini na makamanda wa ngazi za juu wa vikosi vya usalama kwa shabaha ya kumshinikiza Kabila asijitose kwenye kinyang'anyiro cha urais Novemba mwaka huu. Hii ni katika hali ambayo, mwanadiplomasia mmoja mjini Kinshasa ambaye hakutana jina lake litajwe amesema vikwazo vinafaa kutumika kama tahadhari au onyo tu, lakini sio kutekelezwa moja kwa moja. Aidha baadhi ya nchi za Umoja wa Ulaya zinazounga mkono vikwazo, vimesema kuwa machaguo mengine yanafaa kuwekwa mezani kabla ya chaguo la vikwazo. Wadadisi wa mambo wanaamini kuwa, iwapo Marekani pekee itapasisha vikwazo dhidi ya Kongo DR bila kuungwa mkono na EU, yumkini hatua hiyo isizae matunda haswa kwa kuzingatia kuwa, maafisa wengi wa serikali ya Kabila wamewekeza katika nchi za Ulaya. Uchaguzi mkuu nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo umepangwa kufanyika mwezi Novemba mwaka huu, ambapo kwa mujibu wa katiba Rais Kabila hapasi kuwania kiti hicho kwa mara ya tatu mfululizo. Hata hivyo hivi karibuni Mahakama ya Katiba ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, ilitoa uamuzi kuwa Rais Joseph Kabila anaweza kuendelea kusalia madarakani hata baada ya kumalizika muda wa uongozi wake mwaka huu wa 2016, iwapo uchaguzi hautafanyika kwa sababu yoyote ile.